Aliyemwagiwa maji moto apona


Salha Mohamed

NEEMA Wambura (32) aliyeungua kwa kumwagiwa maji ya moto na mumewe ameruhusiwa kutoka hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) huku akitoa ujumbe mzito kwa wanawake wanaotarajia kuolewa.

Tukio hilo lilitokea katika kijiji cha Kyagata, Tarime mkoani Mara, baada ya kuchuma mahindi mawili na kuchoma ndipo akaadhibiwa na mumewe huyo huku akiwa na mimba ya miezi minne.

Akizungumza jana hospitalini hapo, Neema alisema kwa sasa amepona huku akiwashukuru madaktari wa hospitali hiyo na Rais John Magufuli kwa msaada wake kwake.

Alisema wanawake wanapotaka kuolewa waangalie wa kuwaoa ili yasiwakute kama yaliyomkuta yeye, hadi kumwagiwa maji ya moto.

"Mimi ungenikuta pale madhabahuni tunafunga ndoa usingeamini kuwa angenifanya hivi, ni mwanamume aliyekuja kunichumbia akiniambia dada nakupenda na mimi nikakubali, lakini sasa sina matiti," alisema.

Alisema baada ya kumwagiwa maji ya moto alifungiwa ndani na alikwenda kuomba msaada kwa wazazi wake wakamrudisha kwani walishakula mahari.

Alisema alipata msaada wa kufika MNH huku akiwa na hofu ya kutopona akaendelea na matibabu huku viungo vyake vikiwa vimeathirika na moto.

Neema alisema alipata msaada wa matibabu kutoka kwa Rais Magufuli hadi kupona, kwani hata shingo yake ilikuwa haigeuki vema.

"Nilikuwa nasikia maumivu ya kidonda kama kunawaka moto kwa ndani hadi natamani nivue nguo nitupe lakini baada ya Rais kupata taarifa suala hili lilimgusa," alisema.

Aliomba Mungu amsaidie Rais Magufuli na amwepushe na mambo mabaya kutokana na ukarimu aliomfanyia kwa kuokoa maisha yake.

Alisema hadi sasa hajui aliko mumewe baada ya kumdhuru na   huku ndugu na wazazi wake wakimtenga.

Mkuu wa Idara ya Upasuaji MNH, Dk Ibrahim Mkoma alisema walimpokea Neema Julai 6, mwaka juzi akiwa amepewa rufaa kutoka hospitali ya Mkoa wa Mara.

"Alikuwa na jeraha kubwa karibu kifua chote, shingo na kidevu kilikuwa kimeshikana, mkono wa kushoto umeshikana na kifua," alisema.

Alisema baada ya kumfanyia uchunguzi, tulibaini anahitaji upasuaji ambapo wa mwanzo tulimfanyia Julai 21, 2015 iliyotenganisha shingo na kifua na kutenganisha mkono wa kushoto kutoka kifuani na kufunika kidonda.  

Dk Mkoma alisema walichukua ngozi mapajani na baada ya mwezi ngozi bado haikushika vema hadi shingoni, kidevuni na kwapa la kushoto.

"Agosti tulimrudisha chumba cha upasuaji kumpasua sehemu ambayo haikushika vizuri lakini akawa anaendelea vema na hakuwa na kidonda na shingo alikuwa anaweza kunyanyua," alisema.

Alisema Desemba 2015 walimfanyia upasuaji wa tatu wakati huo wakichukua ngozi tumboni na kuweka shingoni ili aweze kuzungusha shingo.

Februari mwaka huu alikuwa anahisi kuumwa mkono na majeraha kuuma na alifika MNH na kupata matibabu huku Rais akitoa msaada.

Alisema Neema aliathirika kisaikolojia na hata kumsababishia kilema cha kudumu kwenye mkono wa kulia kutokana na tishu kuharibika kwa moto.

"Rais ameonesha mfano, watu waige alichokifanya kuanzia kwa mtu binafsi hadi jamii,Watanzania wazuie mambo kama haya kutokea katika jamii zao," alisema.

Alisema jamii inapaswa kupewa elimu ya namna ya kulinda haki za raia hasa wanawake, ili kuepusha yaliyotokea kwa Neema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo