Msiba wa wanafunzi waunganisha itikadi


*Viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa wajumuika kuaga
*Arusha yazizima, vilio, simanzi vyatawala Samia akiongoza

Suleiman Msuya

MSIBA wa wanafunzi 33, walimu wawili na dereva wa shule ya msingi ya Lucky Vincent ya Arusha waliokufa kwa ajali ya basi Mei 5 Karatu, umeunganisha Watanzania ambao kwa pamoja bila kujali itikadi zao za kisiasa jana walijumuika kutoa heshima zao za mwisho.

Wakiongozwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan maelfu ya Watanzania wakiwamo viongozi wa vyama vya siasa, wazazi, ndugu, jamaa na marafiki, walishiriki tukio hilo la kuhuzunisha lililoandika historia mpya ikizingatiwa kuwa ajali hiyo ya barabarani ni ya kwanza kupoteza idadi kubwa ya wanafunzi kwa pamoja.

Viongozi wengine waliohudhuria kwenye tukio hilo ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, Mbunge wa Arusha, Godbless Lema na viongozi wa dini.

Wengine ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango, Waziri wa Elimu wa Kenya, Fred Matiang'i, wabunge, wakuu wa mikoa, wilaya na wengine wengi.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika kwenye uwanja wa michezo  Kumbukumbu ya Shekhe Amri Abeid, Arusha, Makamu wa Rais alisema Taifa limepatwa na mshituko mkubwa na kutaka wazazi na familia zote kuvuta subira kwani Watanzania wako pamoja.

Alisema pamoja na dhana kuwa Mungu ndiye mpangaji katika kila jambo, madereva wanapaswa kuwa makini katika barabara kwa kufuata sheria za usalama barabarani.

Samia alisema watoto hao walikuwa na ndoto nyingi na kwa familia zao, lakini kifo kimekatisha kila kitu, hivyo kinachotakiwa ni kumwomba Mungu.

“Nafahamu walikuwa nguzo na tegemeo kubwa kwa familia zao naomba tutumie nafasi hii kuwaombea ili wapate kuishi kwa amani huko waendako,” alisema.

Alisema Serikali iko na wafiwa katika kipindi hiki kigumu na kuwa tukio hilo limewafungua macho kuangalia maeneo ambayo kwa njia moja au nyingine, yanaweza kuhusika na matukio kama hayo.

“Napenda kuwakumbusha, kuwa kila jambo linalotupata Mungu ana nafasi yake, hivyo hatuna budi kwenda na maandiko matakatifu, ila natoa rai kwa vyombo vyote vya usalama barabarani kuongeza umakini,” alisema.

Alisema wanafunzi hao walikuwa katika kutekeleza majukumu yao ya msingi ya kielimu, jambo ambalo linaongeza maumivu zaidi kwa jamii.

Aidha, alitoa rai kwa madereva kuwa waangalifu katika uendeshaji magari ili kupunguza ajali nchini ili kusaidia kuokoa maisha ya Watanzania wasio na hatia.

Makamu wa Rais aliasa madereva kutotumia kilevi zikiwamo dawa za kulevya wawapo barabarani kwani ni moja ya sababu za ajali zinazotokea.

Makamu wa Rais aliishukuru Kenya kwa kuonesha ushirikiano jambo alilosema linaonesha udugu wa dhati.

“Tumepata faraja kuona ndugu zetu wa Kenya wameshiriki msiba huu, huo ndio ushirikiano wa dhati tunawashukuru sana,” alisema.

Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma alisema ni tukio la kuhuzunisha, kwani watoto hao walikuwa waje kutumikia Taifa siku zijazo ila kimekuwa kinyume.

“Ulikuwepo mwanga ambao unaongoza watoto hawa ila kilichotokea ni tofauti na matarajio yao, kinachotakiwa ni kuwaombea,” alisema.

Akizungumzia msiba huo, Matiang'i alisema walipokea taarifa hizo kwa mshituko mkubwa na kuwataka wafiwa kuvumilia katika kipindi hiki kigumu.

Matiang’i alisema Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta na Wakenya wote wamehuzunishwa na vifo hivyo ambavyo vimechukua nguvukazi ya nchi.

Mbowe alisema Watanzania wanatakiwa kuungana na kushikamana kwa pamoja ili kuwafariji wafiwa.

Alisema msiba huo umeacha pengo kubwa kwa Taifa kutokana na ukweli kuwa vijana hao walikuwa na ndoto za kutumikia kwenye sekta mbalimbali.

Kinana ambaye alionekana hadharani kwa mara ya kwanza baada ya mkutano mkuu maalumu wa chama hicho, aliwaomba wafiwa kuamini kuwa hiyo ni mipango ya Mungu na kila mmoja wao atakutana na kifo.

Profesa Ndalichako alisema sekta ya elimu imepata pigo kubwa kwani ni dhahiri watoto hao walikuwa na ndoto za maisha yao ya baadaye.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alisema kinachotakiwa ni kuombea watoto hao ili waweze kupokewa vizuri Mbinguni.

“Msiba huu ni mgumu sana kuubeba kwa mzazi yeyote, mimi naomba tumpe nafasi Mungu zaidi ili aweze kutenda yake, kwani tupo ambao hatuamini kuwa ni mipango ya Mungu,” alisema.

Viongozi wa dini ambao walipata nafasi ya kuzungumza, waliwataka wafiwa kuamini katika Mungu kwani ndiye anayejua sababu ya vifo hivyo kwani hata wao walio hai hawajui mwisho wao ni lini.

Tukio hilo lilikutanisha maelfu ya wakazi wa Arusha hali ambayo ilisababisha uwanja wa Shekhe Amri Abeid kufurika watu wenye nyuso za huzuni muda wote wa kuaga.

Mapema miili ya marehemu hao ilifikishwa uwanjani hapo kwenye majeneza yaliyobebwa na magari ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo