Lipumba amgalagaza Maalim mahakamani


*CUF yake yaiangusha ya Maalim kuhusu Bodi ya Wadhamini
*Sasa yajipanga kudai gharama za usikilizwaji wa kesi yao

Celina Mathew

Lipumba na Maalim Seif
CUF kambi ya Profesa Ibrahim Lipumba imeibuka kidedea mahakamani dhidi ya ile ya Maalim Seif Sharif Hamad katika kesi iliyohusu uteuzi wa Bodi ya Wadhamini wa Chama hicho kwa kutupwa kwa ombi la Maalim Seif na kuridhia uamuzi wa Lipumba.

Kwa uamuzi huo wa Makahama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam juzi, upande wa Lipumba umesema utadai upande wa Maalim Seif urejeshe gharama ilizotumia wakati wa usikilizwaji wa kesi na kwamba unaendelea na shughuli za chama.

Uamuzi huo wa Mahakama unaweza kufasiriwa kuwa ni ushindi unaoipa nguvu kambi ya Lipumba katika uendeshaji wa CUF ambayo imekuwa kwenye mgogoro wa uongozi, tangu Mwenyekiti huyo atangaze kurejea kwenye nafasi yake.

Lipumba alitangaza kujiuzulu nafasi yake muda mfupi kabla ya Uchaguzi Mkuu, mwaka juzi akidai kupinga Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kumpitisha Edward Lowassa, kuwa mgombea urais kupitia umoja huo akisema ni usaliti.

Hata hivyo, upande wa pili ulieleza kushangazwa na Lipumba ukisema ni mmoja wa walioshiriki kumshawishi Lowassa kujiunga na Ukawa ili awanie urais.

Mkurugenzi wa Habari wa CUF, Abdul Kambaya jana aliwajulisha wanachama na Watanzania kuhusu uamuzi wa Mahakama katika kesi hiyo namba 45/2017 iliyofunguliwa na Bodi ya Wadhamini kutoka upande wa Maalim Seif ukiongozwa na Joram Bashange kuwa imefutwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu. 

“Kesi hiyo ilifunguliwa kwenye Mahakama ya Kisutu na upande unaomtii Maalim Seif dhidi ya upande unaosimamia Katiba ya CUF unaoongozwa na Profesa Lipumba, ukiiomba Mahakama kutoa amri kwa Magdalena Sakaya, Abdul Kambaya, Thomas Malima, Masoud Mhina, Zainab Mndolwa na Salama Masoud, kutojihusisha na shughuli za chama,” alisema. 

Alisema kesi hiyo ilisababisha shughuli za chama kusimama kutokana na baadhi ya viongozi waliopachikwa, ambao si wana CUF kufanya shughuli za chama, huku viongozi wengine wakitangazwa kusimamishwa uanachama na timu ya Maalim Seif.

Alisema baada ya maombi hayo kutupiliwa mbali, walalamikiwa waliruhusiwa kupeleka madai ya kufidiwa gharama za kesi.

“Kwa hiyo waheshimiwa wanachama na wananchi kwa ujumla, tunapenda kuwajulisha kuwa kesi hiyo imekwisha na sisi viongozi wenu tunaendelea kufanya kazi za CUF na tutachukua hatua stahiki, ikiwamo kudai kurejeshewa gharama za chama zilizotumika wakati wa usikilizwaji wa kesi husika,” alisema.

Uamuzi
Juzi, wakili Mashaka Ngole aliweka pingamizi dhidi ya mashitaka hayo, akimwomba Hakimu kuyatupilia mbali.

Kwa mujibu wa Ngole, hatua hiyo ilitokana na vifungu vya Katiba ya CUF kueleza kuwa kesi za kushitaki au kushitakiwa hufunguliwa na Bodi ya Wadhamini ya CUF, lakini wakati kesi ilipofunguliwa, chama hakikuwa na Bodi hiyo.

Alisema wakati kesi ilipofunguliwa, pande zote ndio kwanza zilikuwa zimewasilisha maombi ya usajili wa Bodi mpya na RITA haijasajili upande wowote ule kati ya pande hizo mbili.

Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Wilbert Mashauri mbele ya mawakili wa pande zote mbili, wa walalamikaji, Hashim Mziray na wa walalamikiwa Ngole, alisema ameridhika na pingamizi lililowasilishwa na walalamikiwa dhidi ya walalamikaji.

Hakimu Mashauri alisema waliofungua kesi hawakuwa na sifa zilizoainishwa kwenye Katiba ya CUF kama zinavyoelezwa kwenye Sheria namba 5 inayozungumzia masuala ya uanzishwaji wa vyama vya siasa kuwa lazima viwe na bodi iliyosajiliwa na RITA.

Alisema kwa kuwa RITA haijasajili bodi yoyote, ni dhahiri kuwa walalamikaji hawakuwa na sifa za kisheria kufungua shauri hilo.

Machi 19 kikao cha Baraza la Uongozi la Taifa la CUF upande wa Maalim Seif kilichofanyika Zanzibar, kilipitisha majina ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini na kuyapeleka RITA.

Baada ya kupeleka majina hayo, walipata taarifa kuwa upande wa Profesa Lipumba nao ulishapeleka majina yao RITA.

Aprili 10, Maalim Seif aliituhumu ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania kuwa inashinikiza RITA ipitishe majina ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini yaliyopelekwa na upande wa Lipumba.

Maalim Seif alisema RITA ikipitisha majina hayo, iwe tayari kubeba dhamana kwa yatakayotokea ndani ya chama.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo