Wafutiwa dhamana kwa kumkataa hakimu


Jemah Makamba

HUJAFA hujaumbika. Ndivyo unavyoweza kusema baada ya waumini wa Kanisa la Moravian la Kitunda, Dar es Salaam, kufutiwa dhamana na kupelekwa mahabusu baada ya kudai Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Wilberfoce Luhwago ana mkakati wa kutoa hukumu ya kifungo dhidi yao.

Kutokana na tuhuma hizo, waumini hao waliokuwa nje kwa dhamana, waliombwa na Hakimu huyo kuthibitisha madai yao, lakini baada ya kushindwa aliamuru wafutiwe dhamana.

Washitakiwa hao wakiongozwa na Mchungaji Joachim Mwaseba ni  Mathew Mwakiposa, Kennedy Msangarufu, Geofrey Kibona, Boniface Mwakilasa na Martin Mwiba na walifika mahakamani hapo wakiwa na furaha, lakini wakaondoka wakiwa vichwa chini.

Wakati kesi hiyo ikiendelea, Mwaseba alisimama na kudai kuwa wamekuwa wakisikia maneno kuwa mwisho wa kesi hiyo watahukumiwa kifungo.

"Tumesikia haya maneno sana na tuna hofu juu ya kesi hii kwa hiyo tunaomba tubadilishiwe Hakimu ili tuwe na amani kwani hatuna raha tunawaza kufungwa juu ya kesi hii," alidai Mchungaji huyo.

Kwa kauli hiyo, Luhwago alisema maneno ya Mchungaji huyo yanaweza kugeuka ‘mwiba mchungu’ iwapo atashindwa kuithibitisha Mahakama.

"Mimi natenda haki kwa kufuata sheria na ikiwa hiyo kauli umeisikia hapa mahakamani au kwa mtumishi wa Mahakama, basi naomba umtaje sasa hivi na aitwe hapa aje athibitishe maneno haya,” alisema Luhwago.

Baada ya kubanwa, Mwaseba alidai kuwa maneno hayo aliyasikia  kwa mshitakiwa mwenzake, Msangarufu.

Luhwago alimtaka Msangarufu aiambie Mahakama kama alitamka maneno hayo, naye akadai kuwa hakuyasikia mahakamani, bali kanisani mwao.

“Kwa kuwa mmesikia maneno haya mtaani na hamna uhakika nayo, mtarudi ndani wote ili mkirejeshwa hapa muanze upya utaratibu wa maombi ya dhamana na mngoje jalada lenu kuhamishiwa kwa Hakimu mwingine,” alisema Luhwago.

Washitakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kufanya fujo ndani ya Kanisa wanalosali kwamba Agosti 21 mwaka jana waliingia na kuvunja viti na kuwafanyia fujo waumini wenzao.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo