Majaliwa: Ma-DC kaeni chonjo


Joyce Kasiki, Dodoma

Kassim Majaliwa
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amewatahadharisha wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri wanaopatiwa mafunzo ya uongozi kwamba wataanza kuchukuliwa hatua iwapo watakwenda kinyume cha utendaji wa kazi.

Akifungua programu ya mafunzo ya uongozi kwa wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri kutoka mikoa sita ya Dodoma, Morogoro, Singida, Kigoma, Tabora na Katavi  yanayotolewa na Taasisi  ya Uongozi, Majaliwa alisema awali viongozi hao walikuwa hawachukuliwi hatua kwa sababu walikuwa wanafanya kazi kwa kutumia uzoefu wa mahali walipotoka kabla ya kushika nyadhifa hizo.

"Tunajua katika utendaji wenu mlikuwa mnakabiliwa na changamoto mbalimbali za kiutendaji, lakini kwa kipindi chote cha mwaka mmoja tulikuwa hatuchukui hatua yoyote dhidi yenu ni kwa sababu mlikuwa hamjapatiwa mafunzo wala semina yoyote ya masuala ya uongozi, lakini sasa baada ya mafunzo haya tutaanza kuchukua hatua kwa yeyote atakayefanya kazi kinyume," alisema Majaliwa na kuongeza:

"Kupitia semina hii ya kuwajengea uwezo, tunaamini mtafanya vizuri zaidi kwa kushirikiana na wasaidizi wenu lengo kubwa likiwa ni kuleta maendeleo katika maeneo yenu na Taifa kwa ujumla." 

Majaliwa aliwataka viongozi hao kujenga mazoea ya kusikiliza hotuba za Rais John Magufuli kwani nyingi zimekuwa zikitoka na maagizo wanayopaswa kuyatekeleza kwenye utendaji wao wa kazi sambamba na kufuatilia vipindi vya kitaifa.

Kuhusu mada zitakazotolewa, Majaliwa alisema ni pamoja na utunzaji wa nyaraka za Serikali ambapo alisema nyaraka zenye siri za Serikali zinapaswa kutunzwa kwa umakini mkubwa huku akiwataka wakurugenzi kuwachukulia hatua wale wote watakaohusika katika kuvujisha au kutupa ovyo nyaraka za siri za Serikali.

"Tukisema ni nyaraka za siri tunaamanisha hizo ni siri za Serikali ambazo hazitakiwi kuvuka kwa namna yoyote ile hususan katika kipindi hiki cha utandawazi, haitakiwi kuonekana karatasi lenye siri za Serikali limefungiwa maandazi au bidhaa yoyote, mkurugenzi unapaswa kuchukua hatua haraka kwa mkuu wa idara husika," alisema.

Alizitaja mada nyingine kuwa ni muundo wa Serikali huku akitaka katika eneo hilo wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri kufanya kazi kwa ushirikiano.

Aidha Majaliwa aliwataka wakuu wa wilaya kuusimamia vizuri ushirika na kuchukua hatua kwa wahusika watakaobainika kufanya ubadhirifu katika vyama hivyo bila kusita.

Pia aliwataka viongozi hao kwa umoja wao kuhakikisha wanaondoa changamoto ya migogoro ya ardhi inayojitokeza katika maeneo mengi nchini.

Aliewaasa kuachana na tabia za ulevi kwenye nyumba starehe na kujiheshimu zaidi kwa kuwa wao ni kioo cha jamii.

Awali Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Profesa Joseph Semboja alisema kwa mara ya kwanza taasisi hiyo inatoa mafunzo ya pamoja kwa wakuu wa wilaya na wakurugenzi huku akisema awali walikuwa wakitoa mafunzo hayo kwa wakuu wa wilaya pekee.

Alisema kabla ya Agosti mwaka huu wakuu wa wilaya na wakurugenzi wote nchini watakuwa wamepatiwa mafunzo hayo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji.

Akimkaribisha Waziri Mkuu, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais ,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,  Selemani Jafo alisema lengo la  mafunzo hayo ni kuwapatia mbinu za uongozi viongozi hao ili wazitumie katika maeneo yao ili kuleta tija kwa wananchi na Taifa kwa ujumla. 

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo