Kafulila ataka uchunguzi TISS, Takukuru


Suleiman Msuya

David Kafulila
ALIYEKUWA Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila, amemtaka Rais John Magufuli kuchunguza baadhi ya watumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa alichodai walijenga uhusiano na baadhi ya watendaji kufanikisha wizi wa madini.

Kafulila alisema hayo jana siku moja baada ya Rais Magufuli kupokea taarifa ya Kamati ya Kuchunguza Mchanga wenye Madini ya Dhahabu iliyokuwa chini ya Profesa Abdulkarim Mruma.

Kamati hiyo ilibainisha kuwa katika kontena 277 kuna tani 7.8 za dhahabu zenye thamani ya Sh bilioni 676.

“Namshauri Rais aboreshe TISS kwa kuwa na kitengo cha ujasusi wa kiuchumi kitakachomudu kukabiliana na uharamia wa utoroshaji utajiri wa Taifa,” alisema.

Alisema ipo haja ya kutazama upya Katiba ili ikibainika kuwa Rais yeyote aliyepita alihusika na ufisadi afikishwe kwenye mkondo wa sheria.

Kafulila alisema katika ofisi za viongozi wakuu - Ikulu ndipo vinapotoka vimemo kuruhusu uharamia wa namna hiyo.

“Ni ushauri wangu kwa Rais aruhusu mchakato wa Katiba ili pamoja na mambo mengine, tuangalie mfumo wa ofisi yake kama moja ya vyanzo vya   uozo na uharamia huu,” alisema.

Alisema kampuni hizo za kimataifa zinaiba duniani kote ikiwamo Ulaya na Marekani, isipokuwa huku kwetu zinaiba zaidi kutokana na sera duni, sheria dhaifu, mifumo ya usimamizi dhaifu na udhaifu wa wanaopewa nafasi kwa ujumla.

Aidha, alisema pamoja na changamoto hizo, bado hatua hiyo ya Rais Magufuli inapaswa kuungwa mkono na kila mzalendo huku akisisitiza kuwa ni moja ya malalamiko ya vyama vya upinzani.

 “Naipongeza Kamati kwa kazi iliyotukuka iliyojaa majaribu ya rushwa kubwa, kwani kampuni za madini, mafuta na gesi duniani zina sifa hiyo kama alivyopata kusisitiza Profesa Joseph Stirglitz gwiji wa uchumi na utandawazi duniani,” alisema.

Kafulila alimshauri Rais kuchukua hatua za kisheria za ndani, kwa kuzifikisha kampuni hizo kwenye mahakama za kimataifa kama inavyotamkwa kwenye mikataba ili kuzidai fidia kwa miaka yote ya mikataba yao.

Hali kadhalika alipendekeza mitambo na mali za wawekezaji zishikiliwe mpaka kesi zitapomalizika. “Na hili lisisomeke kwamba ni kukimbiza wawekezaji bali ni kukabili uharamia wa utoroshaji rasilimali ambao hata sheria za kimataifa zinapiga vita,” alisema.

Wakati Kafulila akisema hayo, Mbunge wa Singida Mashariki na Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu alisema hotuba ya Rais Magufuli ni ushahidi mwingine, kama bado kuna shaka, ya mamlaka ya kisheria kwa nchi ambayo anatuingiza kama Taifa.

“Natumia marufuku yake ya kusafirisha mchanga wenye madini nje ya nchi kama mfano,” alisema.

Alisema zaidi ya dhahabu, mgodi wa Bulyanhulu unazalisha pia madini ya fedha, cobalt, shaba na cadmium na ni mgodi pekee nchini wenye madini yote hayo.

Alisema madini hayo kwa mujibu wa Sheria ya Madini na Mikataba ya Uendelezaji Madini (MDAs) waliyopewa na Rais Benjamin Mkapa na kurudiwa na Jakaya Kikwete, ni mali ya wawekezaji.

Mgodi wa Bulyanhulu unachenjua dhahabu kwa asilimia 70 na asilimia 30 iliyobaki inafanyikia Japan ambayo ina mtambo wa hayo madini mengine.

“Ndiyo maana mchanga huo umekuwa unasafirishwa kwenda Japan tangu mwakan 2001. Sasa Rais angewaelekeza wawekezaji wajenge kwanza hicho kiwanda nchini, kabla ya kupiga marufuku usafirishaji mchanga,” alisema.

“Kwa kuzingatia kwamba wawekezaji hawa wanalindwa kisheria na kimkataba, Rais angejadiliana na MDAs ili kufanya mchakato wote ndani kwa ndani,” alisema.

Lissu alisema uamuzi wa Rais unaweza kusababisha agombane na wawekezaji na serikali zao na mabwana wakubwa wa kifedha duniani, ambao ndio wamiliki halisi wa rasilimali hizo.

Watampeleka kwenye mahakama za kimataifa ambazo Mkapa na Kikwete walizikubali kuwa ndizo za migogoro kati yetu na tuliowapa rasilimali zetu.

“Tukipelekwa huko hatuponi, kwa sababu tutakuwa tumevunja mikataba na sheria zinazolinda wawekezaji na hatapata anachokifikiria,” alisema.

Mwanasheria huyo alisema Rais wa Bolivia, Evo Morales alikuta nchi ikiwa na mikataba kama hiyo alipochaguliwa Desemba 2006, cha kwanza alichofanya ni kuiondoa nchi hiyo kwenye makubaliano ya MIGA na kwenye Mikataba ya Uwekezaji (BITs) zilizokuwa zinalazimisha Mahakama ya Kimataifa kwenye migogoro ya uwezekaji.

Kwa upande wake, Venant Rugabela alisema: “Ripoti ni ripoti, uhakika wake ni uhakika wake na utekelezaji ni utekelezaji.” Lakini hoja inarejea kuwa “ni kwa nini wahusika ambao ni wazalishaji hawakuunganishwa katika kamati?”

Mariam Chimile alisema kilichotokea katika taarifa, ni kuonesha dhahiri kuwa nchi imekuwa ikipoteza fedha nyingi ambazo zingepaswa kutoa huduma za kijamii.

“Tumeshuhudia hudumia za afya, miundombinu na nyingine nyingi ambazo zingekuwa nzuri kama madini hayo yamejulikana,” alisema.

Chimile alisema ni wakati mwafaka kwa Serikali kuangalia upya Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 ili kuondoa mkanganyiko.

Ofisa Utawala wa NCCR-Mageuzi, Florian Mbeo alisema ripoti ni nzuri ila suala la msingi ni kutekeleza aliyoyaagiza bila kupepesa macho.

Mbeo alisema pamoja na ripoti hiyo kuwa nzuri, bado kuna changamoto hasa kwenye mikataba ambayo inaoneshwa kukosewa tangu awali na sheria kuwa na ukakasi.

“Tungefurahi kama mikataba ingejulikana kwa kila mwanajamii ili tuweze kutoa maoni, lakini mikataba ile ni siri. Hatujui kilichomo. Wanachukua rasilimali zetu kwa makubaliano ya siri,” alisema.

Alisema haya yote yanayoikuta Serikali lawama zinapaswa kuelekezwa kwao, wabunge na Baraza la Mawaziri.

Aidha, inasemekana taarifa hiyo ambayo alikabidhiwa jana kwa ilisababisha kushuka kwa hisa za kampuni ya uchimbaji madini ya Acacia kwenye Soko la Hisa la London, Uingereza.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo