Zitto akomalia sheria, sera za madini


Suleiman Msuya

Zitto Kabwe
MBUNGE wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe, amesema Tanzania inapaswa kuhakikisha sheria na sera za madini zinalazimisha rasilimali madini kuwa mali ya Watanzania ndipo nchini itanufaika.

Aidha, amesema ni wakati muafaka kwa Taifa kujitoa katika mfumo wa kodi za Kimataifa akiuelezea kuwa umeonesha kunyonya nchi maskini zaidi na kunufaisha zile  tajiri.

Zitto alisema hayo jana wakati akizungumza kwenye kipindi cha Mizani ya Wiki kinachorushwa na televisheni ya Azam Dar es Salaam.

Alisema kwa kuwa Rais John Magufuli ameamua kupigania vita hiyo ni jukumu la kila Mtanzania kupigana hadi kuhakikisha kuwa madini yanakuwa ni mali ya wananchi wa Kitanzania.

Zitto alisema kwa mujibu wa sheria iliyopo inaanisha kuwa baada ya mwekezaji kuingia mkataba na Serikali madini ni mali yake jambo ambalo halikubaliki.

“Hii vita ni vita ngumu ila kwa sababu Rais ameamua kuipigana pamoja na ukweli kuwa anajua jitihada za Serikali iliyopita tunapaswa kumuunga mkono ili tuweze kunufaika.

“Mimi nataka mambo haya mawili yaangaliwe ili kuhakikisha kuwa rasilimali madini inatambulika kama mali yetu kwani kwa sasa ni mali ya mwekezaji,” alisema.

Alisema iwapo sheria inapaswa kumtambua mwekezaji kama mkandarasi kwani kwa sasa inamfanya aonekane ndiye mwenye mali.

Mbunge huyo alisema kwa mujibu ya sheria ya gesi na mafuta mwekezaji ni mkandarasi ambapo akipata bidhaa husika anarejesha gharama yane na katika faida nchi inagawana na mwekezaji kwa sawa au nchi kupata zaidi.

Alisema jambo la pili ni mfumo wa kodi wa kidunia umeweka mazingira ambayo kampuni za Kimataifa zinauwezo wa kuhamisha mapato yake kwenda kwenye visiwa ambavyo kodi zipo chini hali ambayo inachangia wasilipe kodi.

Mbunge huyo alisema mfano mwaka 2011 Kampuni ya Barick wakati huo ambayo kwa sasa ni Acacia ilitoa taarifa ya kupata hasara nchini ila ilionesha kupata faida nchini Uingereza hivyo kulipa kodi kwa Malkia.

Zitto alisema katika kukabiliana na hali hiyo dunia ilianza mjadala wa kuhakikisha kuwa kodi hizo zinapatikana na Tanzania ilikuwa ni mwenyekiti wa mjadala huo ila tangu Serikali ya awamu ya tano iingie madarakani imeonekana kuachwa.

“Ni masikitiko makubwa kwa Serikali ya Tanzania kuacha mjadala ambao tulikuwa tunaongoza wa mfumo wa kodi za Kimataifa ambao ungeweza kutuletea mabadiliko chanya ya rasilimali madini ambayo inaonekana haina faida kwa nchi na wananchi,” alisema.

Mbunge huyo alisema tipoti ya Profesa Abdulkarim Mruma haina jipya katika ripoti ya Jaji mstafufu Mark Boman ambayo ilianisha yote yaliyoanishwa kwa sasa.

Zitto alisema kamati hiyo ilipendekeza miaka tisa iliyopita kuwepon kwa mashine ya uchenjuaji inakuwepo ikiwa ni pamoja na kuwepo sera na sheria sahihi kwa sekta hiyo.

“Nakumbuka nilikuwa masomoni nchini Ujerumani nilirudi kupitisha sheria hiyo ambayo ilipangiwa kutumia wiki moja ila muda haukutosha ikawa wiki mbili na tulishirikisha watu asasi za kiraia ili kutusaidia kupata mkuafaka,” alisema.

Mbunge huyo alisema kwa ushirikiano huo ilikuwa rahisi wajumbe wa kamati ya Bunge ya Nishati na Madini kufanya kazi na kuja na mapendekezo sahihi kuhusu rasilimali hiyo.

Alisema wao kama chama wamejipanga kufanya mjadala mwisho wa wiki hii kuhakikisha jamii inatambua rasilimali madini kwa undani ili kila mtu aweze kufahamu kila kitu.

Kwa upande wake Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Benson Bana alisema ni wakati muafaka wa Watanzania kujitathmini kuwa wana matatizo gani.

Alisema ni vema kuangalia uwezekano wa kutumia wataalam mbalimbali duniani kuhusu rasilimali zake ili ziweze kunufaisha jamii kwa ujumla.

Bana alisema ukifuatilia mfumo wa kutunga sera na sheria za nchi unaonekana kufuata misingi nataratibu zinazohitajika ila kumekuwepo na changamoto ya usimamizi na utekelezaji.

“Wakati mwingine najiuliza tunakwama wapi ila nabakia na tafsiri mbili kwamba kuna mashinikizo ya wazi na yasiyo ya wazi hivyo tunapaswa kujipanga kukabiliana na hali hiyo,” alisema.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo