Watu 7,000 wakamatwa kwa ujangili


Sharifa Marira, Dodoma

ZAIDI ya watu 7,000 wamekamatwa kwa tuhuma za ujangili katika mwaka 2016/17 kutokana na doria iliyofanyika kwa siku 349,103.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe alibainisha hayo bungeni jana alipowasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa Wizara yake kwa Mwaka wa Fedha 2017/18, ambapo alieleza lengo la kuweka doria kuwa ilitokana na matukio ya ujangili na biashara ya haramu ya wanyamapori.

Alisema Idara ya Wanyamapori, TANAPA, NCAA na TAWA, waliendesha doria ndani na nje ya hifadhi hatua iliyofanikisha kukamata watuhumiwa 7,085.

Alisema katika operesheni hiyo, meno ya tembo 129 na vipande 95 vyenye uzito wa kilo 810.03 vilikamatwa sambamba na silaha za kivita 48, silaha za kiraia 150, risasi 1,058, magobori 406, silaha za jadi 22, 307 na roda 120,537.

Profesa Maghembe alitaja vingine vilivyokamatwa kuwa ni pikipiki 189, baiskeli 214, magari 20, ng'ombe 79,831 na samaki kilo 4,043 ambapo kesi 2,097 zilifunguliwa kwenye mahakama mbalimbali na 802 kumalizika huku kesi 262 zenye watuhumiwa 472 zikimalizika kwa wahusika kufungwa jela jumla ya miezi 42,153 na kesi 43 zilizokuwa na watuhumiwa 79 wahusika kuachwa huru.

Alisema kesi 276 zilimalizika kwa watuhumiwa 469 kulipa faini ya jumla ya Sh milioni 452.1 na kesi 966 ziliendelea katika mahakama mbalimbali nchini.

Alieleza kuwa katika kuhakikisha Wizara hiyo inadhibiti ujangili na
biashara haramu ya nyara za Serikali, ilianzisha kikosikazi maalumu, kutumia teknolojia ya ndege zisizo na rubani na mbwa maalumu wa kunusa.

Alisema mwaka 2016/17, doria maalumu za kiintelijensia zilifanyika
kwenye kanda zote za kiikolojia na kubaini wahalifu 906 wa
ujangili ambapo 384 walikamatwa na kufikishwa mahakamani.

Profesa Maghembe alisema taarifa za kiintelijensia zilionesha kuwa
majangili wakubwa wanakimbilia nje ya nchi kujificha wakikwepa mkono wa sheria.

Alisema baadhi ya majangili walisalimisha silaha zao kwa hiari na
alitoa pongezi kwa wajumbe wa kikosikazi, Jeshi la Polisi, kamati za
ulinzi na usalama za wilaya, mkoa na wananchi.

Profesa Maghembe, alisema Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi kwa wanyamapori dhidi ya ujangili na biashara haramu ili kukomesha
vitendo haramu.

Aliliomba Bunge liidhinishe Sh bilioni 148 na kati ya fedha hizo, Sh bilioni 96.9 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh. bilioni 51.8 kutekeleza miradi ya maendeleo.

Bajeti hiyo imeongezeka kwa Sh bilioni 12.80 sawa na asilimia 9.4
ikilinganishwa na bajeti ya 2016/17 na bajeti ya maendeleo imeongezeka kutoka Sh bilioni 17.74 mwaka 2017/18 hadi
Sh bilioni 51.80.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo