Naibu Waziri atajwa mgogoro wa CUF


Mwandishi Wetu

Hamad Yusuph Masauni
MBUNGE wa Jimbo la Konde, Khatib Said Haji  amemtaja Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Yusuph Masauni, kuwa ni mmoja wa watu aliodai wanasababisha mgogoro ndani ya Chama cha Wananchi (CUF).

Isitoshe, akasema hawakumuacha Profesa Ibrahim Lipumba ila walilenga Watanzania kutambua anayofanya na vibaraka wake.

Haji alisema hayo wakati akichangia bajeti ya wizara hiyo ambayo iliwasilishwa na Waziri Mwigulu Nchemba bungeni jana.

Mbunge huyo alisema Masauni amekuwa akishirikiana na kundi la CUF kuhakikisha anakiua chama hicho lakini hatafanikiwa.

Alisema mkakati wa Masauni na kundi la Mungiki ni kuona damu inamwagika ili kukifuta chama hicho.

“Watu wetu, viongozi wetu wameonesha uvumilivu mkubwa. Je, kama juzi yule mpuuzi ambaye alikamatwa pale zisingekuwepo busara zetu si angeuawa, sisi tumedhamiria kulinda amani ya nchi,” alisema.

Haji alisema CUF haimuogopi Lipumba na uwezo wa kumnyoosha wanao. Nia wanayo na nguvu wanayo na wanaweza kutekeleza hilo wakati wowote kama watataka.

Alisema asilimia kubwa ya Watanzania wamebaini upungufu wa Lipumba jambo ambalo linawapa faraja mwisho wake unafika.

Pia alizungumzia sakata la mlundikano wa mahabusu ndani ya magereza kuwa ni moja ya changamoto ambayo inatakiwa kutatuliwa.

Mbunge huyo alitoa mwito kwa Serikali kuondoa watu ambao hawahusiki ili kuondoa msongamano magerezani.

Kwa upande wake, Mbunge wa Tandahimba, Katani Katani (CUF), alisema migogoro ndani ya vyama vya siasa inachochewa na Jeshi la Polisi kwa kuwa kigeugeu katika maamuzi yake.

Mbunge huyo alitolea mfano kuhusu kufanyika mkutano wa ndani wa chama hivi karibuni ambapo Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi CUF, Julius Mtatiro ambaye alizuiwa kufanya mkutano wa ndani mkoani Tanga.

Alisema kinachoendelea ni ishara tosha kuwa Jeshi la Polisi linatumika hali ambayo inaweza kusababisha mgogoro ndani ya nchi.

Katani alisema kitendo cha Waziri Mwigulu kushindwa kusimamia haki katika suala dogo la CUF ni ishara tosha kuwa hata nafasi ya urais ambayo aliiomba alikuwa hatoshi.

“Sisi ni binadamu itafikia mahali uvumilivu utafikia mwisho kwani ambayo yanafanyika hayatendi haki kwa watu wote,” alisema.

Mgogoro wa CUF umedumu takriban miezi sita sasa ambapo Lipumba na kundi lake linavutana na kundi lingine ambalo linatambulika kuwa ni la Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad kuhusu uhalali wa Lipumba kurejea katika nafasi ya uenyekiti.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo