Serikali yalaani mama kuunguza mtoto


Mary Mtuka

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu
WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, imelaani kitendo cha mkazi wa kata ya Rudete mkoani Geita, ambaye ni mama wa kambo, kumchoma moto mtoto wa miaka mitatu akituhumiwa kuiba chakula alichoachiwa baba yake.

Katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana, Wizara ilisema tukio hilo linakinzana na kaulimbiu ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Familia mwaka huu, ambayo pamoja na mambo mengine, inasisitiza wazazi na walezi, kutekeleza wajibu wao wa kuimarisha malezi kwa ajili ya ustawi wa watoto katika familia na jamii kwa jumla.

"Katika kutekeleza utoaji haki za mtoto na ustawi wake, wadau   wanaotoa huduma kwa mtoto wanasisitizwa kusimamia upatikanaji wa haki zote za msingi katika familia na jamii, ikiwamo haki ya kuishi, kulindwa, kuendelezwa, kushirikishwa na kutobaguliwa," ilieleza.

Wizara inawataka wananchi kutoa ushirikiano wa kufichua wanyanyasaji dhidi ya watoto kwa kutoa taarifa kwenye Mamlaka husika, ili wahusika wa ukatili wachukuliwe hatua.

Aidha, Wizara ilitoa maelekezo kwa maofisa maendeleo na ustawi wa jamii kuhakikisha mtoto huyo anapewa huduma ya matibabu haraka ili kumrejesha katika afya njema.

“Hata hivyo kwa kuwa jukumu la ulinzi na usalama wa mtoto linatekelezwa kwa ushirikiano mkubwa na Polisi, tunaamini suala hilo linafuatiliwa kuhakikisha watuhumiwa wa vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya huyo mtoto wanapatikana," ilisema taarifa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo