Polisi wanawake waamshwa wajipange


Mwandishi Wetu

MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan amewataka askari Polisi wanawake kutoka Shirikisho la Majeshi la Polisi Kusini mwa Afrika (SARPCCO) kushiriki kikamilifu oparesheni za kijeshi zinazofanyika kwenye ukanda huo kukabiliana na uhalifu.

Samia alitoa kauli hiyo alipofungua mafunzo ya siku tatu ya polisi wanawake kutoka nchi wanachama wa SARPCCO Dar es Salaam jana.

“Vyeo haviji tu ni lazima polisi wanawake muoneshe mnaweza, ili muweze kupandishwa vyeo na kupata nafasi za uongozi kwenye majeshi yenu. Mshiriki operesheni za kijeshi Kusini mwa Afrika,” alisema Samia.

Aliwaambia muda wa kulalamika kuwa hawapandishwi vyeo umepitwa na wakati na sasa lazima wachape kazi na kuonesha wanaweza majukumu wanayopangiwa ili wapande vyeo.

Kuhusu utendaji kazi wa polisi wanawake, Makamu wa Rais aliwataka   kutumia mkutano huo kujadili kwa kina namna ya kuondoa changamoto zinazorudisha nyuma utendaji kazi wao.

Alisema kama polisi wanawake wataacha majungu na kujenga umoja na mshikamano miongoni mwao, watafikia malengo yao haraka hasa katika kushiriki kikamilifu mapambano dhidi ya uhalifu ikiwamo biashara ya dawa za kulevya.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Masauni alisema ana imani mafunzo hayo yatasaidia polisi hao kuimarika ipasavyo katika utendaji kazi wao.

Aliwahimiza polisi hao wanaopata mafunzo hayo kwenda kuelimisha wenzao mipango na mikakati waliyoweka ya kulinda raia na mali zao nchini mwao.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo