Vita ya Lwenge, Kitwanga yafikia patamu


*Ni ile iliyoanzia bungeni kwa sakata la maji

Suleiman Msuya

Charles Kitwanga
MWAKA mmoja baada ya Rais John Magufuli kutengua uteuzi wa aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga, mbunge huyo wa Misungwi ameibuka na kusema anashangaa kuona Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Gerson Lwenge akiendelea kuwa waziri.

Aidha, amesisitiza kuwa iwapo watu wa kijiji cha Ihelele kilichopo jimboni kwake hawatapatiwa maji katika siku za karibuni, atawaongoza kwenda kuzima mtambo wa kupeleka maji katika maeneo mengine.

Kitwanga aliyasema hayo jana wakati akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu kutoka Dodoma, akimjibu Lwenge ambaye juzi wakati akijibu hoja za wabunge walizozitoa wakati wakichangia bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha wa 2017/18, alimtaka mbunge huyo kuhama CCM kama anaona Serikali haijafanya lolote katika wilaya ya Misungwi.

Lwenge alisema Kitwanga alikuwa Waziri wa Mambo ya Ndani katika Baraza la Mawaziri la Kwanza la Serikali ya Awamu ya Tano, michango yake kuhusu tatizo la maji aliitoa mithili ya mtu anayeonesha kuwa Serikali ya CCM haijafanya chochote.

“Sasa nataka nimuulize Kitwanga kama yupo hapa kwamba hayo ni mamneo yake au ya wananchi? Kama ni wananchi nitamuambia nini kimefanyika Misungwi, kwani hata juzi tumetia saini mikataba ya maji na mwenyekiti wa halmashauri aliyekuwepo kwa ajili ya kupeleka maji kutoka Ziwa Victoria kwa zaidi ya Sh.bilioni 38,” alisema Lwenge.

Katika maelezo yake ya jana, Kitwanga alisema waziri Lwenge alipaswa kuja na majibu ya lini maji yatapatikana Ihelele na si kumuambia ahame chama kwani katika swali lake hakuhusisha kuhama chama.

Mbunge huyo alisema haiwezekani maji yasipatikane katika wilaya hiyo wakati eneo hilo kuna mradi wa kupitisha maji kwenda mkoani Tabora.

”Hivi kweli mimi naweza kuhama CCM? na je nikihama nitaacha kudai mahitaji ya watu wa Misungwi? Nadhani hajaelewa hoja yangu ndio maana nashangaa ni vipi hadi leo anaendelea na uwaziri,” alisema.

Alisema changamoto ya maji inayowakabili wananchi wake haina mjadala, ni lazima ipatiwe ufumbuzi na kama waziri anaona kuna utani watamuonesha dhamira yao ya kuzima mtambo.

Kitwanga alisema wao hawana shida na maji hata kama yatapelekwa hadi jijini Dar es Salaam, ila lengo la wananchi hao ni kutaka maji hayo pia yawafikie.

“Maji yanatoka kwetu lakini hatuna. Hatutaki kuwanyima watu maji, lakini na sisi tupate na kama hilo halioni basi mawazo yake yana matatizo na atajuta kuzaliwa,” alisema.

Aidha, alisema anasikitishwa na mitazamo ya baadhi ya mawaziri kuona kuwa wabunge wa CCM wanaosemea jambo fulani ni wapinzani.

Kitwanga alisema waziri anapaswa kutambua kuwa ni jukumu la kila mbunge kufikisha kero za wananchi wake Serikalini ili zitatuliwe na sivinginevyo.
Wakati wa kuchangia bajeti ya wizara ya maji na umwagiliaji alisema ataandaa wananchi zaidi ya 10,000 kwenda kuzima mtambo wa kuleta maji Shinyanga na Tabora.

Kwa upande mwingine, Kitwanga alisema hahofii mtu yoyote ambaye anadhamira ya kugombea ubunge katika jimbo hilo na watapambana wakati ukifika.

Akichangia katika bajeti ya maji hivi karibuni, Kitwanga alisema atahamasisha wananchi wa Misungwi wapatao 10,000, waende kuzima mitambo katika chanzo cha maji ili wote wakose.

Alisema shida yake si bajeti ya wizara hiyo na hatoweka ngumu wakati wa upitishwaji wale, ila atakachokifanya ni kuwachochea wananchi hao huku akionekana kukasirishwa zaidi baada ya Lwenge kusema wilaya hiyo ina maji.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo