Bunge lataka NGOs zilizoko Loliondo zifutwe


Sharifa Marira, Dodoma

KAMATI ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, imeishauri Serikali
kufuta asasi zote zisizo za Serikali (NGOs) zinazofanya shughuli zake kwenye Pori Tengefu la Loliondo na kusajili chache kwa masharti na vigezo vya kulinda na kuhifadhi rasilimali za nchi.

Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Atashasta
Nditiye, alipowasilisha maoni ya Kamati hiyo wakati wa
uwasilishwaji wa Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii.

Alisema kuna NGOs zaidi ya 25 ambazo zote zimejikita katika utalii, uhifadhi na utetezi wa wananchi katika pori hilo.

Alisema asasi hizo nyingi zinamilikiwa na wanasiasa na kufadhiliwa
na taasisi za kimataifa ambazo Kamati haina uhakika na lengo lao kufadhili uhifadhi kwa kuwa ni washindani wa kibiashara ya utalii na uhifadhi.

‘’Kamati imegundua kuwa NGOs hizi kwa kiasi kikubwa zimekuwa
zikichangia mgogoro unaoendelea katika eneo hilo baina ya Serikali na
wananchi kwa kuwapotosha juu ya wajibu wao kwa uhifadhi wa
Serikali yao,’’ alisema Nditiye.

"Kuna sintofahamu ya matumizi ya ardhi na masharti maalumu yanayotakiwa kwenye mapori yetu hususan kwa wawekezaji na
wananchi wanaozunguka hifadhi na mapori tengefu," alisema
Nditiye.

Alisema Kamati hiyo imeishauri Serikali kuweka wazi masharti ya
uwekezaji na uwindaji katika maeneo ya mapori na uhifadhi  ili kuondoa migogoro inayoendelea kwenye Pori Tengefu la Loliondo na
maeneo mengine.

Aidha, Mwenyekiti huyo alisema katika kuiongeza mapato Serikali,
Kamati imeshauri kuongeza juhudi na mbinu za kisasa katika kukabiliana na ujangili na biashara haramu ya wanyamapori, kwa kutoa mafunzo ya kupambana na maharamia.

Pia kuimarisha ulinzi na uhifadhi wa wanyamapori walio hatarini
kutoweka, wakiwamo faru, tembo na kudhibiti usafirishaji wa pembe za ndovu kwenye bandari na viwanja vya ndege.

Nditiye, alisema Serikali ina wajibu wa kushirikiana na Mamlaka husika kubaini mbinu za kupunguza vifo vya wanyamapori
wanaokufa kwa kugongwa na magari kwenye barabara zinazopita ndani ya hifadhi.

Pia kuongeza juhudi za kusimamia sheria na utaratibu kwa
kushughulikia watakaokutwa na hatia ya ujangili kwa kesi zao kusikilizwa haraka na kutoa adhabu kali.

Serikali ilitakiwa pia kuimarisha ulinzi wa ghala la kuhifadhia nyara
za Taifa na kuweka kamera za usalama, vifaa vya kugundua moto
na kutoa mafunzo ya kujikinga na kupambana na moto.  

Kwa upande wa sekta ya misitu na nyuki, Serikali ilitakiwa kuimarisha
ulinzi katika misitu ili isivamiwe na shughuli za binadamu zisizo endelevu ukiwamo uvunaji haramu, ufugaji, uchomaji mkaa na
kilimo.

Pia kuandaa mipango endelevu kwa ajili ya makazi ya watu hasa katika
miji mikubwa inayozunguka hifadhi na inayokua kwa kasi.

Mwenyekiti alisema Serikali inapaswa kuongeza rasilimaliwatu
katika Taasisi ya Utafiti na Misitu (TAFORI) ili kuiwezesha
kuanzisha na kusimamia majaribio ya utafiti kikamilifu.

Pia Kamati ilishauri Serikali kuharakisha mchakato kuamua
kwa tija ili kuokoa gharama inazoingia kumtunza Faru Fausta ambaye yuko kwenye uangalizi maalumu kutokana na maradhi aliyonayo na umri wake.

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni iliishauri Serikali kumaliza mgogoro wa Loliondo uliodumu kwa miaka 30 na kugharimu maisha ya wananchi kutokana na jamii ya wafugaji wa bonde la Loliondo.

Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Esther Matiko alisema mgogoro
huo unachochewa na pande tatu zinazosigana ambazo ni wawekezaji, Serikali na wananchi .

Alisema mgogoro huo ulichochewa na kampuni ya Otterlo Business Corporation (OBC) kupewa kibali cha uwindaji na kumilikishwa
ardhi kinyume na sheria za wanyamapori namba 12 ya Mwaka 1974.

Matiko aliitaka Serikali itoe majibu ya tuhuma zinazoikabili
OBC na Serikali na kuja na kauli kuhusu mgogoro huo, kwani kila kukicha viongozi wake wanakinzana, jambo linalofanya wananchi waendelee kupata shida.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe aliomba Sh 148,597,946,000 aliishukuru familia yake kwa kumfariji hata
katika sakata la Faru John akisema alikuwa katika kipindi kigumu.


Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo