Mihogo ya sumu yaua mtoto, 6 hoi


Leonce Zimbandu

MTOTO wa miaka mitano amefariki dunia na watu wengine sita wa familia moja kukimbizwa katika zahanati ya Kivule wakiwa hoi, wakidaiwa kula mihogo yenye sumu.

Janga hilo lilitokea juzi eneo la Uthamini, mtaa wa Mbondole, manispaa ya Ilala na kuzua taharuki kwa majirani na baadhi ya watu waliofika nyumbani kwa Chacha Fyefye kushuhudia.

Mmoja wa mashuhuda hao ambaye ni dereva wa bodaboda, Daud Mseti, alidai kwamba alipokuwa kituoni alifuatwa na mtu na kumweleza afuatane naye kumchukua mgonjwa ili kumpeleka hospitali.

Alidai baada ya kufika nyumbani kwa Chacha, alikuta watoto watatu wamelazwa chini na kuwabeba kwenye pikipiki na kwenda nao zahanati ya Kivule.

“Tulipofika Kivule, muuguzi wa zamu alitupokea vizuri na kutoa huduma, baada ya muda mfupi mama na watoto wengine walifika katika zahanati hiyo wakiwa hawajitambui,” alidai.

Alidai kuwa ingawa vitanda katika zahanati hiyo vilikuwa vichahche, lakini wagonjwa hao walipokewa na kupewa huduma na kunusuru afya zao.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Mbondole, Thomas Nyanduli alidai kuwa hali hiyo inasikitisha na kutaka wananchi kuchukua hadhari ya kununua vitu ovyo na kula na kuwataka wananchi kutoa taarifa haraka ili hatua zichukuliwe wanapopatwa na matatizo kama hayo.

Alidai, Mama Chacha ni mfanyabishara wa mboga, ambaye husafirisha mboga alfajiri kwenda kuuza maeneo ya Viwege, hivyo alipomaliza kuuza bidhaa hiyo, alinunua mihogo hiyo bila kujua.

“Hatuwezi kuthibitisha kama ilikuwa ni sumu ya namna gani, lakini mtoto mmoja amepoteza maisha baada ya kula mihogo hiyo na wengine wamekimbizwa zahanati na baadaye katika hospitali ya Amana kwa ajili ya vipimo,” alisema.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ilala, Salum Hamduni alisema hana taarifa ya tukio hilo, lakini akaahidi kulifuatilia kujua ukweli.

“Sina taarifa, nitafute baadaye lakini kwa sasa sina jibu la moja kwa moja,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo