Wapinzani wakataa Muswada wa Haki ya Kutoa Taarifa


Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni
Wabunge wa Upinzani wameishukia Serikali wakitaka iondoe bungeni au kuufanyia marekebisho makubwa Muswada wa Sheria ya kupata taarifa walioubatiza jina la ‘Sheria ya Mkakati kwa Mambo yanayoendelea nchini’.

Wamesema Muswada huo uliotarajiwa kupitishwa jana jioni baada ya kujadiliwa kwa siku mbili utapitishwa kwa sababu ya wingi wa wabunge wa CCM, lakini umejaa kasoro na unalenga kuminya vyombo vya habari, watoa taarifa na kulinda ufisadi unaoweza kufanywa na watendaji wa Serikali.

Wakizungumza katika mjadala huo, wabunge hao waliainisha baadhi ya vifungu, kikiwamo cha nne, sita, 10 na 19 kupendekeza viondolewe, huku Mbunge wa Tandahimba (CUF), Katani Ahmed Katani akisema sheria hiyo inalenga kubana watu katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2020.

Baadhi ya kasoro walizoainisha katika sheria hiyo, ni pamoja na adhabu kali ya kifungo kwa mtu atakayetoa taarifa za uongo, kuzuia mtu asiye raia wa Tanzania kupata taarifa, taarifa kutolewa na mamlaka husika ndani ya siku 30 na sheria kutumika Tanzania Bara pekee.

Kauli za wabunge hao zilipingwa na wabunge wa CCM, waliosisitiza kuwa Muswada huo ni mzuri na unahitaji marekebisho madogo na kupingana na kauli ya wenzao wa Upinzani kuwa wadau hawakushirikishwa.

Akizungumzia kifungu cha sita cha sheria hiyo, Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema) alisema hakielezi nani anayethibitisha kuwa taarifa itakayozuiwa kutolewa inalenga kulinda usalama wa Taifa, kwa maelezo kuwa jambo hilo litakuwa kichaka cha kuficha taarifa muhimu zinazoibua ukweli kuhusu mikataba ya kifisadi.

“Uko ufisadi wa kutisha ulioibuliwa na taarifa za uchunguzi, leo hii tunataka kuzuia wanaotusaidia kupata taarifa kwa sababu Serikali inataka kutengeneza kichaka cha kujibana ili taarifa muhimu zisipatikane,” alisema.

Huku akisisitiza kuwa Muswada huo utaua uhuru wa vyombo vya habari na kuvunja haki ya kikatiba ya kutoa na kupata taarifa, alisema kifungu kinachoeleza kuwa taarifa itatolewa ndani ya siku 30 si sahihi kwa sababu haiwezi kuwa na maana kama haikutolewa wakati mwafaka.

Alibainisha kuwa sheria hiyo kuelezwa kuwa itatumika Tanzania Bara pekee wakati Mtanzania anatambulika kama raia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni sahihi, huku akihoji kitendo cha wabunge kutoka Zanzibar kushiriki mjadala huo wakati hawataitumia sheria husika.

Kauli hiyo ya Selasini iliungwa mkono na Katani aliyesisitiza kuwa kifungu cha sita kutoa mamlaka ya chombo cha uchunguzi kuchunguza bila kueleza uchunguzi utafanyika lini, ni jambo linalohitaji kutazamwa kwa makini.

Mbunge wa Viti Maalumu, Devotha Minja (Chadema) alisema sheria hiyo inabagua wageni kupata taarifa wakati Tanzania hupata taarifa nyeti kutoka nchi zinazosaidia kubaini ufisadi, huku akitoa mfano jinsi nchi zilivyofichua sakata la ununuzi wa rada.

Alisema adhabu ya kifungo cha miaka 15 hadi 20 kwa mtu atakayetoa taarifa ya uongo ni kubwa na inafanya watu washindwe kutoa taarifa za awali na kusubiri watoa taarifa wanaotambulika kisheria.

Wakati Minja akisema maoni yaliyotolewa na wadau kuhusu Muswada huo yameachwa, Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Mollel (CCM) alisema wadau wote walishirikishwa huku akisisitiza kuwa lazima kudhibiti utoaji taarifa, akitolea mfano habari zilizochapishwa katika gazeti la kila wiki kwamba kifaru cha Jeshi kimeibwa.

Katika majadala huo, Mbunge wa Ulanga Mashariki Goodluck Mlinga (CCM) akitumia lugha za vijembe alisema si kila jambo zuri linalowasilishwa bungeni linalenga kudhibiti wapinzani.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo