Tetemeko linapoahirisha ziara ya Magufuli Zambia



Mashaka Mgeta

JUZI, Ikulu ya jijini Dar es Salaam ilitoa taarifa mbili, moja ikielezea ziara ya Rais John Magufuli nchini Zambia, baadaye ikaelezea kuahirishwa kwake.

Ziara hiyo iliyopangwa ‘kuchukua’ siku tatu, huku ratiba ikihusisha kushiriki kuapishwa kwa Rais Edgar Lungu, ilifutwa ili Rais Magufuli ashughulikie kadhia ya kuibuka kwa tetemeko la ardhi lililotokea na kugharimu maisha ya Watanzania zaidi ya 16.

Ninamuomba Mwenyezi Mungu awapumzishe katika usingizi wa Amani wote waliotutoka, na kuwaondolewa maumivu majeruhi wa janga hilo.

Lakini tukio la Rais Magufuli kuahirisha ziara yake nchini Zambia kutokana na kadhia ya tetemeko ni jambo jema, lile ambalo linaashiria na kuchagiza ari kwa Watanzania na dunia kujali utu wa mtu.

Ingawa Rais Magufuli amewakilishwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, ile kuwapo kwake nchini wakati huu taifa likiomboleza vifo, majeraha, upotevu wa mali na kadhia nyinginezo zinazotokana na tetemeko hilo, inatia faraja.

Ni faraja ambayo haipaswi kutokana na asili ya tukio, kwamba ni tetemeko ambalo halikutarajiwa, ni faraja ambayo haipaswi kuwa katika msingi wa namna watu walivyoangukiwa na kuta, wakapoteza maisha ama kujeruhiwa.

Ni faraja ambayo haipaswi kutokana na kutafuta na ‘kuziteka’ hisia za watu. La hasha. Rais Magufuli, kwa hatua hiyo anauleta utu wa mwanadamu katikati ya mioyo ya watu.

Utu wa mtu unapojengwa kwa raia wa taifa kama Tanzania, inakuwa kichocheo chema cha ‘kusimika’ umoja wa kitaifa, ushirikiano, utulivu na amani ya kweli.

Kwa hiyo wakati Rais Magufuli akiwasilisha kielelezo hicho kwa kujali tatizo lililoikabili nchi badala ya kwenda kugongesha glasi za shangwe kwenye jiji la Lusaka kusherehekea kuapishwa kwa Rais Lungu, inabidi tafakari iliyopo ivuke mipaka kutoka Bukoba mkoani Kagera.

Kwamba wapendwa wetu kadhaa wamepoteza maisha kutokana na tetemeko la ardhi. Janga hilo ni la asili ambalo ni vigumu kuzuilika hata kwa mataifa yenye nguvu kubwa za kijeshi na uchumi ulioimarika.

Lakini ukweli unabaki kuwa janga limeyachukua maisha ya watu wetu kama wanavyopoteza maisha ndugu wengine ama itakavyokuwa kwetu kupitia magonjwa kama malaria, vifo vya watoto na wajawazito, japo kutaja kwa uchache.

Kwa hiyo tunaweza kujiweka kando na uwezekano wa kudhibiti janga la asili kama tetemeko lililotokea Bukoba. Lakini kama taifa inabidi utashi wa kisiasa na dhamira ya mtu mmoja mmoja vielekezwe katika kulifanya taifa lisiingie katika simanzi kama iliyopo sasa, kwa kudhibiti vifo vinavyoweza kuzuilika.

Kuvizuia vifo visivyotokana na majanga ya asili ni pamoja na kuwapo kwa sera, sheria, kanuni na taratibu bora, zikichangiwa na ushiriki wa kila kada ya kijamii badala ya kuwaachawatawala ili mwisho wa siku
wasutwe ama kunyooshewa vidole.

Tetemeko la Bukoba linapomuibua Rais Magufuli kuahirisha ziara yake huko Zambia, linakuwa fundisho kuwa Tanzania ni moja na Watanzania ni wamoja.

Kwamba tunapozungumzia tetemeko hilo, waathirika wake si wakristu tu, waislamu tu, watu wa kabila fulani ama au chama cha siasa.

Ni Watanzania kwa asili yao, tumeathirika, tumepoteza ndugu, mali na miundombinu kuharibika. Kumbe sasa kupitia maisha ya ndugu waliolala katika usingizi wa milele, ama wale wanaoumia katika majeraha makali wengine wakipoteza viungo vyao, Watanzania wana wajibu wa kuiona nchi ni zaidi ya maslahi ya tofauti zilizopo.

Kwamba kama ilivyo kwa tetemeko, taifa ‘likitikiswa’ kwa namna nyingine yoyote, waathirika wake ni Watanzania na si vinginevyo.

Mathalani, kama uchumi ukiyumba kiasi cha raia kushindwa kumudu gharama za maisha, ni Watanzania wote watakaoathirika. Kama ni kupotea kwa amani na utulivu uliopo, waathirika ni raia wote katika upande wowote wa nchi.

Ama kama ambavyo taifa limeletwa pamoja kupitia shida zinazotokana na tetemeko la ardhi, Watanzania wanahitaji kuwa pamoja katika maisha ya kawaida, kuanzia ngazi za familia hadi taifa.

Haiwezekani Watanzania wakalilia kutokuwapo hali ya kuridhisha nchini, pasipo kujitafakari katika hali ilivyo katika ngazi tofauti za kijamii. Kwa mfano, Rais Magufuli anapoahirisha ziara nje ya nchi, inatoa tafisri gani kwa baba ama mama anayekabiliwa na shida kwenye familia yake, lakini akaendelea ‘kutumbua maisha’ kwenye maeneo ya starehe ama vilezi?

Rais Magufuli ameonyesha njia, kwamba haifai. Ninaamini kwamba kwa tukio la tetemeko hilo, nchi italetwa pamoja, ili tofauti za Watanzania ziwe katika hoja na si mapigano.

Kwa maana mapigano yanaleta mauti yasiyotofautiana na yanayoshuhudiwa kwa ndugu waliokufa kutokana na tetemeko la ardhi, kasha nchi kuingiwa na simanzi. Tanzania haihitaji simanzi hasa zinazotokana na tofauti za kijamii kama siasa, imani nakadhalika. Tanzania haihitaji kutojali utu wa mwanadamu, hivyo kusudio jema lipate kujengwa kuanzia ngazi ya familia hadi taifa.

Mwenyezi Mungu awapumzishe ndugu zetu waliokufa katika tetemeko la ardhi huko Bukoba-
AMINA.
0754691540
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo