Ajali nyingine yaua 13 Mwanza


WATU 13 wamepoteza maisha na wengine 11 kujeruhiwa kwenye ajali ya magari mawili yaliyogongana kwenye makutano ya barabara kuu za Mwanza-Shinyanga na ya kutoka kijiji cha Mwamaya wilayani hapa.

Ajali hiyo ilitokea jana saa 12:15 asubuhi ikihusisha basi dogo aina ya Toyota Hiace na basi kubwa la abiria lililokuwa likitoka Mbeya kwenda Mwanza.

Akizungumza jana kwa simu kuhusu ajali hiyo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi alisema Toyota Hiace ikitoka Mwamaya ikiendeshwa na Kurwa John, iligongana na basi la Super Shem.

Msangi alisema katika ajali hiyo watu 10 walipoteza maisha papo hapo wakiwamo watoto wawili, ambapo majeruhi watatu walifariki dunia wakiwa njiani na kwenye hospitali ya Ngudu wilayani Kwimba ambako walipelekwa kutibiwa majeraha waliyopata.

Kamanda alisema kwenye ajali hiyo watu 11 walijeruhiwa na kukimbizwa kwenye hospitali hiyo ya wilaya lakini 10 kutokana na hali zao kuwa mbaya walihamishiwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando (BMC).

Alidai kuwa chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa Hiace ambaye alikuwa kwenye mwendo kasi na bila kuchukua hadhari aliingia kwenye barabara kuu na kukumbana na basi hilo lililokuwa likiendeshwa na Kisoka Shirima.

“Hili basi la Super Shem lilikuwa likitoka Mbeya kuja Mwanza lakini usiku lilipumzika Shinyanga na liliondoka asubuhi kufika Mwamaya kwenye makutano na barabara kuu ya Mwanza-Shinyanga likakutana na Hiace ambayo dereva wake aliingiza bila hadhari likagongwa na kusababisha watu 10 kupoteza maisha papo hapo na majeruhi,” alisema Kamanda Msangi.

Alieleza kuwa dereva wa Hiace, anadaiwa kutoroka baada ya ajali hiyo huku wa Super Shem akijeruhiwa pekee yake kati ya waliokuwa kwenye basi hilo.

Alisema dereva huyo alibanwa na usukani lakini bado polisi wanawachunguza majeruhi waliopo hospitali ili kumbaini dereva anayedaiwa kutoroka kama ni miongoni mwao.

Kamanda Msangi alisema baadhi ya miili ya marehemu hao ambao wengi ni wa kijiji cha Mwamaya imetambuliwa na majeruhi mwingine anadaiwa alipelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Misungwi.

Hii ni ajali ya pili mbaya kutokea ndani ya siku mbili baada ya ile ya usiku wa kuamkia juzi mkoani Njombe iliyotokana na kupinduka kwa basi la kampuni ya New Force na kusababisha vifo vya watu 12 na wengine 28 kujeruhiwa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo