Lipumba aiondoa CUF Ukawa


Fidelis Butahe

MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, anayetajwa kurejeshwa madarakani na Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi ametangaza kujitenga na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), akisema kwa sasa hana nafasi, bali ana kazi ya kukijenga upya chama chake.

Kauli hiyo ya Lipumba imekuja siku moja baada ya gazeti hili kuripoti kuwapo hatari ya Ukawa kufa, ambapo msomi huyo wa Uchumi amesema kazi ya kwanza atakayofanya ni kuiimarisha CUF na si kukumbatia vyama vya Ukawa.

Lipumba alitoa kauli hiyo jana asubuhi katika mahojiano maalumu na JAMBO LEO, siku mbili baada ya kurejea madarakani kwa kauli ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, kumtambua kuwa Mwenyekiti halali wa CUF kisheria.

“Ushirikiano utakuwa wa kimkakati… lengo langu kubwa ni kujenga chama na kuleta maridhiano ya kisiasa Zanzibar maana tumepata majeraha makubwa. Ukawa ni Katiba ya Wananchi na tutashirikiana nao (Ukawa) litakapokuja suala la kusimamia maoni ya Katiba ya Jaji Warioba (Joseph). Ukawa si chama rasmi kinachotambuliwa,” alisema Profesa Lipumba katika mahojiano hayo.

Hatua hiyo ya Lipumba inaweza kupunguza nguvu za Ukawa inayojipanga kuwania umeya katika manispaa nne za Jiji la Dar es Salaam za Kinondoni, Ubungo, Temeke na Kigamboni.

Uchaguzi huo unakuja baada ya kugawanywa kwa manispaa za Kinondoni iliyozaa Ubungo na Temeke iliyozaa Kigamboni, huku mvutano ukitarajiwa kuwa mkali iwapo kutaibuka madiwani watakaomwunga mkono Lipumba ndani ya CUF.

Kauli hiyo ya Profesa aliyerejea kwenye wadhifa wake baada ya kujiuzulu kutokana na alichoeleza kuwa ni kutofautiana na uongozi wa chama hicho, pia imekuja siku moja baada ya wenyeviti wa vyama vinavyounda Ukawa, kutaja mambo manne yanayokwamisha malengo yao.

Viongozi hao, Freeman Mbowe (Chadema), James Mbatia (NCCR- Mageuzi) na Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi wa CUF, Julius Mtatiro walitaja changamoto hizo kuwa ni Dola kutumika kugawanya vyama hivyo, kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara, kupuuzwa kwa maoni ya Rasimu ya Katiba ya iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na migogoro ya ndani inayovikumba vyama hivyo.

Ukawa iliundwa na vyama hivyo pamoja na NLD mwaka 2013 wakati wa Bunge Maalumu la Katiba baada ya kususa kushiriki vikao vya Bunge hilo, kwa maelezo kuwa maoni ya wananchi yaliyokuwa kwenye Rasimu ya Katiba ya iliyokuwa Tume yaliondolewa na CCM kuweka maoni yake.

Mwaka mmoja baadaye, vyama hivyo vilisaini makubaliano ya ushirikiano, ukiwamo wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana namasuala mengine, huku msingi mkuu ukiwa ni kutaka Katiba ya wananchi.

Katika maelezo yake, Profesa Lipumba alisema baada ya kujiuzulu wadhifa wake, CUF ilidorora huku taswira ya chama hicho ikitoweka machoni mwa watu.

“Kazi inayonikabili hivi sasa ni kurejesha wanachama wetu pamoja ili kujenga chama na kutibu majeraha. Baada ya mimi kung’atuka chama kimedorora na taswira yetu haisikiki. Chama hakifanyi uenezi na kuna wilaya nyingi hazina uongozi. Sitafukuza mtu CUF zaidi ya kutaka kurekebisha mambo,” alisema.

Alipoulizwa atafanyaje kazi na wanachama wasiomwunga mkono alisema, “msisome watu wanachoandika kwenye mitandao ya kijamii. Wanachama wengi wananiunga mkono wala sina wasiwasi katika hilo hasa Bara, ila Zanzibar kuna ‘sumu’ imemwagwa ila tutapeana taarifa ili kujenga chama.”

Alibainisha kuwa kama angekuwa haungwi mkono angekosa nguvu ya kutaka kurejea kwenye chama hicho, na kusisitiza kuwa lengo lake lilikuwa kustaafu, lakini wanachama wengi walimfuata nyumbani kumtaka arejee kwenye uongozi.

Akizungumzia viongozi wa CUF wanaompinga, akiwamo Naibu Katibu Mkuu, Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui na Mtatiro, alisema ni vijana wadogo kwenye siasa wasiomsumbua na kubainisha kuwa kama hawana tamaa basi wanatumika.

“Huyu (Mazrui) wakati sisi tunafanya maandamano Zanzibar kudai mambo ya msingi yeye alikuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyabiashara wa Zanzibar la Dk Salmin (Amour- Rais mstaafu wa Zanzibar),” alisema.

“Hawa vijana wadogo wadogo ambao hawajui michango yangu katika chama wamekuwa wakitoa kauli zao tu… wapo akina Mtatiro ambao nilimteua kuwa Naibu Katibu Mkuu, hajagombea nafasi yoyote ndani ya chama ila kwa kuteuliwa,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo