Mbowe azuru eneo la tetemeko


WAKATI Rais John Magufuli akiahirisha safari ya Zambia ili kushughulikia athari za tetemeko la ardhi Kagera, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesitisha shughuli zake na kwenda mkoani humo kupata taarifa za kina juu ya athari zilizotokea.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Chadema, Tumaini Makene, Mwenyekiti huyo pia atatembelea maeneo yaliyokumbwa na tetemeko hilo pamoja na sekondari ya Ihungo ambayo Mwenyekiti huyo alisoma kidato cha tano na sita.

“Kutokana na madhara makubwa, vikiwamo vifo, majeraha na uharibifu wa makazi uliosababishwa na tetemeko la ardhi Jumamosi, Mwenyekiti wa Chama Taifa amelazimika kukatisha ratiba ya shughuli za kikazi na yuko safarini kwenda Kagera,” alisema.

Makene alisema Mbowe akiongozana na viongozi wa Chadema na Serikali, waatanzia ziara mjini Bukoba na baada ya kupata taarifa ya kina juu ya athari zilizopo hadi sasa, atapita maeneo yaliyokumbwa na tetemeko hilo.

Alisema mojawapo ya maeneo ambayo Mwenyekiti atakwenda kujionea athari kubwa zilizotokea ni pamoja na sekondari Ihungo ambayo Mwenyekiti huyo alisoma, ambapo inaelezwa kuwa shule hiyo ni moja ya maeneo yaliyoathiriwa sana na janga hilo.

“Mwenyekiti atafika kuwapa pole na kuwafariji waathirika wa tetemeko, waliofiwa, waliojeruhiwa na ambao walilazimika kujihifadhi kwenye viwanja vya mpira baada ya makazi yao kuharibiwa,”alisema Makene kupitia taarifa hiyo.

Aliongeza kuwa chama hicho kinaendelea kutoa pole kwa waathirika wa tetemeko hilohuku kikitoa mwito kwa Watanzania kuendelea kuguswa na kuwa pamoja na waliokumbwa na maafa hayo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo