Matetemeko 5 yatokea nchini mwaka huu

CHUO KIKUU cha Dar es Salaam (UDSM) kimesema matetemeko matano makubwa ya ardhi yametokea nchini mwaka huu. Aidha, kimezindua kampeni harambee ya kuchangia fedha na huduma za kibinadamu kwa waathirika wa tetemeko la ardhi lililotokea Kagera Jumamosi.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Mkuu wa Idara ya Jiolojia ya UDSM, Dk Elisante Mshiu alisema kati ya matetemeko yaliyotokea mwaka huu, manne yalitokea ndani ya miezi 10 iliyopita. Alitaja matetemeko hayo kuwa la kwanza lilitokea Dodoma Julai 7 likiwa na ukubwa wa 5.1 kwa kipimo cha Richter, Mtwara 5.2, Manyara 4.8 na Kigoma 4.3 huku kubwa zaidi likiwa ni la Kagera la 5.9.

“Tetemeko hili la Kagera ambalo kiini chake kilikuwa ni kilometa 40 lilitokea karibu na mkondo wa Magharibi wa bonde la Ufa la Afrika Mashariki na kutokana na uhalisia wa kijiolojia na kijiografia, matetemeko zaidi yanatarajiwa kutokea,” alisema.

Hata hivyo, alifafanua kuwa matetemeko hayo ni ya kawaida na kwamba kwa mwaka hutokea matetemeko 150 hadi 1,500 duniani yakiwa na ukubwa wa kati ya Richter 4.5 hadi 5.2.

“Matetemeko ya ardhi hutokana na msuguano na mgandamizo wa miamba ambayo ikifikia hatua ya kutohimili migandamizo husababisha tetemeko,” alisema.

Aidha, alifafanua kuwa kupitia tetemeko hili wataalamu watapata fursa ya kujadili na kuangalia kama nchi inaweza kupata matetemeko mengine, huku akisisitiza kuwa hakuna kifaa kinachoweza kutabiri matetemeko.

Alisisitiza kuwa maeneo yaliyo katika Bonde la Ufa Afrika Mashariki, yamo hatarini kukumbwa na matetemeko.

Aliihadharisha Serikali ya mkoa wa Dodoma, kutumia wataalamu wakati wa mchakato wa ujenzi wa majengo, ili kupata utaalamu wa majengo yatakayohimili matetemeko hayo.

Akizungumzia harambee, Kaimu Makamu Mkuu wa UDSM, Dk Bashiru Ally alisema itaendeshwa kwa mwezi mmoja na kutaka wachangiaji kutumia akaunti ya University of Dar es Salaam Self Insurance namba 040103001175 kupitia benki ya NBC.

“Tunahamisha Watanzania wenzetu kujitokeza kuchangia kusaidia waathirika,” alisema. Pamoja na harambee hiyo, chuo kinataendelea kutoa elimu na taarifa sahihi kwa umma kuhusu tetemeko la ardhi, kwani ni moja ya nyenzo muhimu za kukabiliana na majanga ya asili.

“Tutafanya hivi kwa kutoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu, kufanya utafiti na uhamasishaji Watanzania kuongeza mshikamano katika kipindi cha shida na raha,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo