Seif amtimua Lipumba CUF


Suleiman Msuya na Elizabeth Mwaseba

BARAZA Kuu la Uongozi la Taifa la CUF, limemfukuza uanachama aliyekuwa Mwenyekiti wake Profesa Ibrahim Lipumba likieleza kujiridhisha kwamba amekiuka Katiba ya chama.

Baraza hilo limetaja makosa mengine kuwa ni Lipumba kuvamia Ofisi Kuu ya CUF, kuongoza makundi ya wahuni yaliyopiga walinzi wa chama, kuvunja ofisi za chama na kufanya uharibifu wa mali za chama siku ya Septemba 24 mwaka huu.

Pamoja na viongozi wakuu wa chama hicho kutopokea simu kuthibitisha taarifa hiyo, baadhi ya wajumbe ambao hawakupenda majina yao yatajwe, walisema ni kweli Lipumba amefukuzwa kama mwanachama na si kiongozi.

“Baraza limejiridhisha kuwa kikao cha Kamati ya Utendaji kiliitishwa kwa kufuata masharti ya Katiba na hakikuvunja masharti yoyote ya kuitisha Baraza Kuu na limejiridhisha kuwa Profesa Lipumba alifikishiwa barua yenye tuhuma zake, lakini kwa makusudi alikiuka kuitika mwito wa Baraza na hivyo kupoteza haki ya kusikilizwa,” ilisema taarifa hiyo iliyotumwa na Ismail Jussa kwenye ukurasa wake wa Facebook jana jioni.

Taarifa hiyo ilinukuliwa pia na Julius Mtatiro ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi wa CUF.

Aidha, taarifa hiyo ilisema Baraza lilikataa ushauri na mwongozo wa Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kwa chama kwa sababu ulikiuka matakwa ya Sheria ya Vyama Vya Siasa, hauna mantiki na mashiko ya kisheria na unakiuka matakwa ya Katiba ya CUF.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa Baraza Kuu linasisitiza kuwa Kamati ya Uongozi iliyoundwa ndiyo inayotambulika kikatiba hadi atakapochaguliwa Mwenyekiti mpya wa CUF.

Aidha, mmoja wa wajumbe ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema katika mkutano huo uliofanyika kwa takribani saa tatu akidi ilitosheleza, ambapo kati ya wajumbe 62 waliopaswa kuhudhuria, 45 walifika huku watatu wakitoa udhuru.

Alisema wajumbe wawili ambao ni Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti, hawakuhudhuria kwa sababu chama hicho hakina viongozi hao, baada ya Lipumba kujiuzulu na Makamu Mwenyekiti Juma Duni Haji kuhama chama.

Mjumbe huyo alisema wajumbe saba walisimamishwa kwenye kikao cha Baraza kilichofanyika Agosti 28 na wajumbe watano hawakutoa taarifa ya kutohudhuria.

Alisema katika kikao hicho, ajenda zilikuwa tatu; kufungua kikao, kumjadili Lipumba na uharibifu wa mali za ofisi na barua ya Msajili ya kuelekeza CUF kumtambua Lipumba kama Mwenyekiti.

Juzi Kamati ya Uongozi ya CUF ilimwandikia bara Lipumba kumwita mbele ya Baraza Kuu ahojiwe, lakini alisema hawezi kwenda kwa sababu Mwenyekiti wa Kikao ambaye ni Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad hayupo.

Wakati akitoa majibu hayo, Seif aliwasili Zanzibar juzi usiku na jana akashiriki kikao hicho ambacho kilifanya uamuzi wa kumfukuza.

Wakati uamuzi huo ukitolewa, Profesa Lipumba aliitisha mkutano wa wanachama Dar es Salaam kuwaambia wananchi sababu za kurudi kwenye uongozi wa chama hicho tofauti na awali kuwa alijiuzulu.

Profesa Lipumba alieleza sababu zilizomfanya ajiuzulu kuwani chama hicho kumezwa na Ukawa, huku Chadema ikichanua. “Lakini nilishangaa kuona wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka jana, Chadema ikipita kila jimbo na kusema Ukawa ni Chadema tu, hivyo kuigawa Tanganyika na Zanzibar kimafungu,” alisema.

Alisema sababu nyingine ni kuwa wakati wa kikao, Katibu Mkuu Maalim alipata kusema kuwa Freeman Mbowe na Lipumba hawamhitaji Dk Wilibrod Slaa hivyo kumtaka yeye agombee urais.

Wakati wa kipindi cha uchaguzi aliuliza kama wamejiandaa kuweka wagombea wakati yeye ni kiongozi wa chama. Alisema CCM ilishaambiwa kila kitu na Katibu wa chama chao, hivyo wana CUF hawana mgombea wa chama na wanategemea makapi ya CCM.

Mwenyekiti alisema yeye bado ni mwanachama wa CUF na ataendelea kuwa Mwenyekiti, hivyo wanachama wasiwe na wasiwasi.

“Mimi sina matatizo na Katibu Mkuu na tunamsubiri aje kuendelea na kazi yake. Akae akijua atakaporejea atanikuta mimi Mwenyekiti na tutaendelea na kazi, kwani meza yake na viti vipo, lakini ajue kabisa kuwa nina nafasi yangu ya uenyekiti wa chama,” alisema Lipumba.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo