Ukawa hatarini kufa


* Mbowe, Mbatia waeleza kirusi kilichoandaliwa kuiua

Fidelis Butahe

TAKRIBANI miaka miwili baada ya vyama vinne vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kutiliana saini ya makubaliano saba ya ushirikiano, wenyeviti wake wametaja changamoto nne zinazokwamisha malengo yao.

Hata hivyo, viongozi hao wamesisitiza kuwa uhai wa umoja huo kuelekea ushindi kwenye uchaguzi mkuu mwaka 2020, unategemea zaidi kuaminiana kwa viongozi wa vyama vya CUF, Chadema, NCCR- Mageuzi na NLD vinavyouunda.

Kwa nyakati tofauti wenyeviti wa vyama hivyo vilivyoandika historia mpya tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, wameliambia JAMBO LEO kwamba bila upinzani imara ni ngumu kuitikisa CCM na hila zinafanyika kuwagawanya.

Changamoto za Ukawa Walitaja changamoto hizo kuwa ni dola kutumika kuvigawanya vyama vinavyounda Umoja huo, kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara, kupuuzwa kwa maoni ya Rasimu ya Katiba ya iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na migogoro ya ndani inayovikumba vyama hivyo.

Wenyeviti hao, Freeman Mbowe (Chadema), James Mbatia (NCCR-Mageuzi) na Julius Mtatiro ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya uongozi ya CUF, wamesema wataimarisha Ukawa hadi dakika ya mwisho licha ya kuwa Katiba na sheria za vyama vya siasa, vinakiukwa kwa lengo la kuwabana.

Oktoba 26 mwaka 2014, viongozi wakuu wa vyama hivyo vitatu pamoja na NLD, walisaini makubaliano hayo katika viwanja vya Jangwani, huku msingi wa umoja huo ukitokana na kuachwa kwa maoni ya wananchi yaliyokuwa katika Rasimu ya Katiba ya tume hiyo iliyokuwa ikiongozwa na Jaji Joseph Warioba.

Katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka jana, vyama hivyo vilisimamisha mgombea mmoja wa urais na kumuunga mkono, huku vikiachiana baadhi ya majimbo na Kata.

Mbowe

“Msingi mkuu wa Ukawa ilikuwa kupigania Katiba ya Wananchi, mpaka sasa kumekuwa na mgogoro mkubwa kuhusu mtizamo na tafsiri ya siasa ni nini kiasi kwamba chama kimoja kimoja kufanya kazi ya siasa imekuwa taabu achilia mbali kufanya siasa kwa pamoja,” alisema Mbowe.

“Tulitarajia kurudi kusaka Katiba ya Wananchi, ambayo ilitegemewa kutoa mwanya wa vyama vya siasa kuungana kitu ambacho kwa katiba ya sasa (inayopendekezwa) inakataza. Hicho kimekuwa kikwazo kikubwa kwa upinzani kuimarika na wenzetu wanatumia wingi wao kukataa umuhimu wa kuwa na mazingira ya kisheria na kikatiba kwa vyama kuongeza nguvu.”

Mbowe alitolea mfano jinsi Katiba ya Zanzibar ilivyovunjwa kwa kuundwa kwa Serikali ya ‘mezani’ ya Umoja wa Kitaifa, “wenzetu hawana utamaduni wa kuheshimu sheria. Katika mazingira kama hayo unazungumziaje mustakabali wa Ukawa? Tunazungumziaje wakati hata kufanya siasa ni tatizo.”

Kuhusu mvutano ulioibuka CUF huku aliyekuwa mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba akirudi katika wadhifa wake, Mbowe alisema ni jambo la kustaajabisha.

“Yeye (Lipumba) alikuwa mtu wa kupinga Ukawa sasa umoja wetu unakwendaje sasa? Kuna changamoto nyingi za kuzifanyia  kazi kabla ya kujua mwelekeo wetu. Lengo la kuimarisha upinzani lipo pale pale, tutajitahidi kwa nguvu zetu kama Chadema kuhakikisha tunaendelea na ushirikiano wetu,” alisema.

Mbatia

Akizungumzia umoja huo, Mbatia alisema kwa muda mrefu dola imekuwa ikifanya hila kuvigawa vyama vya upinzani, huku akitolea mfano yaliyotokea NCCR-Mageuzi baada ya mwaka 1995 na yaliyokikumba CUF.

“Ukawa hatuhitaji kanuni zituongoze, tunachohitaji ni ushirikiano na kuaminiana ambako ndio kulizaa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar. Hata Nyerere (Mwalimu Julius) na Karume (Amani Abeid) waliaminiana na kuunganisha vyama baadaye sheria ikafuata.”

Alisema kitendo cha wabunge wa vyama vinavyounda umoja huo kuaminiana bungeni, ikiwa ni pamoja na kususia vikao vya chombo hicho cha kutunga sheria kudai kile alichokiita ‘jambo muhimu kwa maslahi ya wananchi’, ni ishara nzuri.

“Ndani ya vyama vyetu wapo baadhi ya wanachama hawapendi umoja huu, hivyo kama kiongozi usipoangalia wapi umoja unataka kwenda hatuwezi kufika…, nawashauri wenzangu tuangalie maslahi mapana ya Watanzania kuliko maslahi binafsi za kila chama,” alisema Mbatia.

“Tulivyokwenda katika uchaguzi, moja ya malengo tuliyokuwa nayo pamoja na ushirikiano ni kuhakikisha kuwa kabla ya 2020 tunakuwa na chama kimoja cha siasa, lakini hatukushinda, ila lengo hilo litatimia kama tutaaminiana.”

Mtatiro

“Ukawa ni jukwaa kubwa zaidi la kisiasa baada ya uchaguzi wa mwaka jana. Uwepo wetu uliambatana na makosa mengi ya kujifunza, kunafikiana, kutoaminiana, kuchezeana kete za kisiasa…, hata kama vyama vilinafikiana na kuzungukana bado wananchi waliamini umoja wetu, kuelekea 2020 tutarajie uimara zaidi,” alisema.

“Kwa sasa Ukawa tunaogopwa zaidi. Tazama Rais Magufuli kwa sasa hataki kuona viongozi wa vyama vya Ukawa wakizunguka kufanya shughuli za kisiasa. Woga huo ukupe salamu kuwa sisi tunaendelea kuwa tishio,” alisema.

“Kwa sasa Rais anafanya makosa kadhaa ambayo kisiasa ni makubwa, ndiyo anazidi kuipa nafasi. Rais akimaliza miaka yake mitano bila viwanda, ajira, uchumi kuzidi kuporomoka, Ukawa itakuwa lulu.”

Alisema kwa sasa CUF inaendelea kujiimarisha ili ikifika mwaka 2019 chama hicho kiwe kimejizatiti ipasavyo katika kutengeneza ushirikiano imara.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo