Makonda amefungua njia kuelekea uboreshaji afya



UCHAMBUZI HURU


Mashaka Mgeta

MWISHONI mwa wiki iliyopita, wananchi kutoka maeneo tofauti za nchi walishiriki upimaji afya ulioratibiwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ukafanyika kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam.

Idadi ya wahitaji wa vipimo vya afya ikazidi matarajio, kwamba kutoka watu 3,000 waliotarajiwa ikafika 15,000.

Kwa tafsiri rahisi, afya ni ukamilifu wa binadamu kimwili, kiakili na kijamii na kutokuwepo kwa maradhi. Akizungumza kwenye hafla ya mazishi ya aliyekuwa Mwandamizi Mwandamizi wa Habari, marehemu Simon Kivamwo, Makonda akasema kutokana na ongezeko hilo, alilazimika kuomba madaktari 90 kutoka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) ili ‘kuongeza nguvu’.

Inafaa kumpongeza Makonda kwa ubunifu huo, licha ya changamoto nyingi zilizojitokeza katika utekelezaji wa mpango wa kupima afya za watu.

Mpango wa upimaji afya huo unaweza kutafsiriwa kwa namna nyingi tofauti, ingawa katika ujumla wake, tafsiri hizo hazipaswi kubezwa, bali kumpongeza Makonda na watoa huduma walioshiriki katika upimaji na tiba kwa waliopaswa.

Pasipo kuzijadili changamoto ama namna utekelezaji wa mpango ulivyofanyika, ongezeko la wahitaji wa upimaji afya limeibua taswira ya namna Taifa linavyokabiliwa na changamoto zinazohusiana na afya za watu.

Ni wazi kwamba kuna tatizo. Watu wengi kwenye maeneo tofauti ya nchi wanaathirika kwa kuugua maradhi wasiyoyabaini, hususan kwa kukosa tiba inayostahili. Kwa sababu hospitali za rufaa katika mikoa tofauti, ama zile za wilaya, vituo vya afya na zahanati, zinapokosa madaktari ama watoa huduma wenye sifa zinazotambulika kwa mujibu wa sera ya afya, haipaswi kujiaminisha kwamba taifa ‘lipo salama’.

Kumiminika kwa wahitaji kutoka maeneo ya mijini na vijijini kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja hakupaswi kuchukuliwa kama mafanikio ya utekelezaji wa mpango husika, basi kuwa kielelezo cha kuwapo utashi wa kisiasa, utakaowezesha kutambuliwa zaidi kwa umuhimu wa sekta ya afya kwa maisha ya watu.

Kama ilivyo kwa mataifa mengi hususani barani Afrika, sekta ya afya haipewi kipaumbele sana hata katika ahadi zinazotolewa nyakati za kampeni za Uchaguzi Mkuu. Inaelezwa ‘kijuu-juu’ kuhusu azma ya kuiboresha sekta hiyo, lakini ahadi nyingi hazijikita katika mkakati usiotiliwa shaka, kwamba unajenga mazingira bora ya kuiboresha sekta ya afya.

Mathalani, sera ya afya ya mwaka 1990 iliyopitiwa mwaka 2007, imeweka bayana dira na makusudio ya kuwa na zahanati kwa kila kijiji na kituo cha afya kwa kila kata. Je, tangu kupitishwa kwa sera hiyo na marekebisho yake kadha wa kadha, ni hatua gani Taifa limepiga katika kuhakikisha kuwa kila kijiji kina zanahati na kata kuwa na kituo cha afya?

Ni ukweli ulio dhahiri kwamba vipo vijiji vyenye zanahati na kata zenye vituo vya afya. Lakini tathmini inayohusisha muda, rasilimali, vipaumbele na nguvu kazi, vinawiana na idadi ya zahanati na vituo
vya afya vilivyopo?

Hata pale ambapo kuna zahanati, vituo vya afya na hospitali katika ngazi za wilaya, mkoa na taifa, kuna idadi inayotosheleza ya wataalamu na vifaa tiba?

Je, mfumo wa tiba unaotumika nchini ni rafiki kwa mwananchi hasa mlipa kodi masikini, akiwamo anayeisikia sauti ya Makonda ikihamasisha mpango wa vipimo bila malipo, yu radhi hata kutembea umbali mrefu kwa saa kadhaa, afike Mnazi Mmoja?  Haifai kukosoa mfumo ama hali ya huduma za afya nchini, lakini haipaswi kujiliwaza na kutembea kifua mbele kwamba taifa ‘lipo salama’ katika upatikanaji wa huduma hizo.

Mpango wa upimaji afya jijini Dar es Salaam ni wa muda mfupi, ambao pamoja na kuwa wenye tija, lakini hauwezi kukidhi vigezo vya kuwa endelevu na kuwafikia wahitaji wanaostahili.

Ni kwa mtazamo huo, Serikali, wadau wa maendeleo, watunga sera, wawakilishi wa umma na wadau wengine, wanapaswa kuunganisha nguvu za pamoja na kuiwezesha sekta ya afya iwe yenye manufaa kwa mujibu wa haki inayomstahili kila raia.

Kuwapo majengo ya zahanati, vituo vya afya na hospitali hakutakuwa na manufaa kama taifa halitawekeza katika kuwaandaa wataalamu na kuwaandalia mazingira bora ya kufanya kazi nchini badala ya kukimbilia nje.

Wataalamu wanapaswa kujulikana kwa idadi inayohitajika, hata kama ni kuwalipia kwa vipindi maalum ili ufike wakati nchi iwe na uwiano unaotakiwa kikanda na kimataifa, kwa daktari mmoja kutibu wagonjwa. Kwa upande mwingine, taifa linapaswa kuwekeza katika tiba na vifaa tiba katika ngazi za zahanati, kituo cha afya na hospitali.

Mambo ya msingi yatakaposhindwa kufikiwa na badala yake nchi ikajiridhisha kwa mipango ya muda mfupi, hata kama ina tija kama ya upimaji afya ulioratibiwa na Makonda, bado hatutakuwa katika njia nzuri ya kuboresha huduma hizo na kuzifanya kuwa rafiki wa raia wengi. Hongera. Paul Makonda.

0754691540
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo