JPM: Mkataba wa TICTS, TPA urekebishwe


RAIS John Magufuli ameibua mambo matatu makubwa, likiwamo la kuagiza mazungumzo ya kurekebisha mkataba wa Kampuni ya Kimataifa ya Kuhudumia Shehena ya Kontena Bandarini (TICTS), ili uwe na tija kwa Taifa.

Hatua hiyo ya Rais imekuja miezi mitano baada ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali(CAG), Profesa Juma Assad, kubaini Aprili kwamba kampuni hiyo imevunja mkataba na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).

Kampuni hiyo inadaiwa kubadili umiliki wa asilimia 51 za hisa kutoka kampuni ya Ictis zilizoko Titcs kwenda Hutchison International Port Limited (HPH) na kuikosesha mapato TPA.

Titcs iliingia mkataba na TPA mwaka 2000 wa upangishwaji eneo la kontena la TPA Kurasini Dar es Salaam, lakini ripoti ya CAG ilibainisha kuwa siku 20 baada ya mkataba huo wa miaka 10 kusainiwa, hisa hizo zilihamishiwa HPH.

Katika ziara ya Rais Magufuli bandarini Dar es Salaam jana, ambayo waandishi wa habari walizuiwa bila maelezo ya kina, tofauti na kuambiwa ni mkutano wa ndani kati yake na wafanyakazi wa TPA, Rais alikutana na wafanyakazi hao huku wafanyakazi wasiokuwa na vitambulisho licha ya kuvaa vizibao vya TPA wakikataliwa kuingia ndani na kurudi ofisini kuendelea na majukumu yao.

Mbali na kuuzungumzia mkataba wa Ticts, pia aliiagiza TPA kununua mashine nne za kukagulia mizigo bandarini hapo na mita za kupimia mafuta.

Kuhusu kampuni hiyo, Rais alisema TPA inapaswa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili kurekebisha mkataba huo. Magufuli alisema mkataba wa Ticts na Serikali ulilenga kunufaisha pande zote, hivyo ni vema ukaangaliwa upya ili kutoa manufaa stahiki.

Ticts inafanya kazi ya kupakua mizigo kwenye magati namba nane hadi 11 ambapo kwa muda mrefu mkataba wake umekuwa ukilalamikiwa bila ufumbuzi.

Kuhusu mashine, Rais aliipa TPA miezi miwili kununua nne ambazo zitasaidia kudhibiti uhakika wa mizigo ambapo kwa sasa kuna udanganyifu.

Pia alitoa agizo hilo baada ya kubaini kuwa kati ya mashine nne za ukaguzi wa mizigo zilizopo, ni mbili tu ndizo zinafanya kazi na hazina uwezo wa kukagua mizigo yote inayotoka na kuingia nchini kupitia Bandari hiyo.

“Kwa hiyo nawaagiza TPA, na Waziri (Profesa Makame Mbarawa) na TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania) mpo hapa hakikisheni mnanunua mashine nne za kukagulia mizigo ndani ya miezi miwili, na ikifika miezi mitano muwe mmenunua sita, ni lazima mizigo yote ikaguliwe kwa mashine,” aliagiza Rais Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli aliiagiza TPA kuhakikisha kuwa inanunua mita za kupimia mafuta yanayopakuliwa kwenye meli, hiyo ikiwa ni baada ya kubaini kuwa mita zilizopo hazifanyi kazi.

“Naagiza tena TPA kuharakisha mchakato wa kununua mita mpya na kuzifunga eneo hilo ili kudhibiti ukusanyaji wa mapato ya kodi ya mafuta,” alisema.

Dk Magufuli aliitaka TPA kujipanga kujenga bandari kavu (ICD) Ruvu, Pwani na kuachana na bandari kavu zilizoanzishwa na watu binafsi Dar es Salaam ambazo zimekuwa zikitumika kukwepa kodi.

Akizungumza na wafanyakazi baada ya kumaliza kutembelea bandari, Rais aliwatoa shaka na wafanyakazi wengine serikalini, kuwa uhakiki wa vyeti unaoendelea nchi nzima hauna lengo la kuwafukuza kazi.

Alisema unafanyika ili kukabiliana na tatizo la wafanyakazi hewa ambao sasa wamefikia 17,500 na pia kuondoa wafanyakazi wanaotumia vyeti bandia.

Wakati huo huo, Rais Magufuli amemwapisha Dk Zainab Chaula kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi). Dk Chaula amejaza nafasi iliyoachwa wazi na Dk Deodatus Mtesiwa ambaye amestaafu. Kabla ya kuteuliwa Dk. Chaula alikuwa Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, Dodoma.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo