Wasomi wazungumzia safari za nje za JPM


Mwandishi Wetu

Dk John Magufuli
KAULI ya Rais John Magufuli kuwa hataki kusafiri nje ya nchi kwa sababu akifanya hivyo mambo yataharibika kwani anaendelea kunyoosha nchi, imeibua hisia tofauti kwa wasomi na wanasiasa.

Baadhi yao wanasema inaweza kuashiria kutojiamini wengine wakisema inakiuka Katiba huku baadhi wakisema yuko sahihi.

Akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya siku tatu mkoani Pwani, juzi Rais Magufuli wilayani Kibaha, alisema amepata mialiko zaidi ya 50 lakini amekataa ili asimamie mipango aliyoahidi kutekeleza kwa wananchi.

Magufuli alikwenda mbali zaidi na kusema amesitisha hata posho, semina, warsha na safari kwa watumishi wa umma, kama hazina tija kwa Taifa, ili kila mtu ajikite kujenga Taifa na kuleta maendeleo.

Akizungumzia kauli hiyo, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino (SAUTI), Profesa Mwesiga Baregu alisema kauli hizo zinaashiria kuwa Rais Magufuli hajiamini kwa sababu amekuwa akifanya uamuzi unaokandamiza jamii.

Profesa Baregu alisema katika nchi inayoendeshwa kwa misingi ya Katiba na demokrasia, Rais hawezi kuhofia kusafiri kwa kisingizio cha kujenga nchi.

“Mimi nadhani hajiamini, naweza kuliunganisha hili na kufungia vyama vya upinzani kufanya mikutano ya hadhara, kwani kila mtu anaona kinachoendelea nchini, kwa kukandamiza demokrasia, tunaona madiwani, mameya na viongozi wetu wanavyokamatwa,” alisema.

Aidha, alisema upo uwezekano Rais haamini watu wa karibu naye na pengine Chadema inampa hofu, kutokana na idadi ya kura ilizopata kwenye Uchaguzi Mkuu uliopita, hivyo anaongoza kwa kuiweka nchi kwenye wasiwasi.

Mhadhiri huyo alisema pia uamuzi wake wa kukaa nchini kwa kisingizio cha kusimamia mipango, inaleta picha ya umimi katika kila jambo.

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Richard Shukia alisema anaunga mkono jitihada za Rais Magufuli katika kusimamia ujenzi wa nchi, lakini akatoa angalizo kuhusu kauli hizo, akisema zinakiuka Katiba na miongozo ya nchi.

Dk Shukia alisema kwa mujibu wa Katiba, hakuna kinachoharibika kwa Rais kufanya safari za nje ya nchi kama atakuwa anaaminiana na wasaidizi wake.

“Mimi naamini anapaswa kujenga imani na wasaidizi wake na asifike mahali akaona bila yeye hakuna kinachowezekana jambo ambalo si sawa,” alisema.

Alisema kauli za viongozi zinakwenda mbali, hivyo Rais anapaswa kuwa makini katika kauli zake na kutambua kuwa urais ni taasisi si mtu.

“Tunapaswa kuamini kuwa tunafanya kazi kama familia, naamini hata katika familia, baba akiondoka anatakiwa kuamini kuwa mambo yatakwenda,” alisema.

Dk Onesmo Kyauke ambaye ni Mhadhiri Mwandamizi wa UDSM, alisema kauli ya Rais isitafsiriwe kwa ujumla wake, kwa kuwa amekuwa akisisitiza kwamba anataka kujenga mfumo wa Serikali yake.

“Yeye ndiye mwamuzi wa nani aende nani asiende, hivyo si lazima aende yeye na kinachohitajika ni alichotakiwa kwenda kukifanya kimepata mtu au la,” alisema.

Dk Kyauke alisema kwa Tanzania watu wote wanafanya kazi kwa niaba ya Rais, akitolea mfano wa Waziri Mkuu anayefanya kazi kwa maagizo ya Rais tofauti na Kenya ambako Naibu Rais anafanya anayotaka kwa mujibu wa Katiba.

Aliyekuwa Mbunge wa Arumeru Magharibi, Goodluck ole Medeye alisema Rais amedhamiria kujenga Tanzania anayoitaka, hivyo katika kutekeleza hilo ni lazima awepo nchini muda wote.

Medeye alisema uamuzi wa Rais Magufuli ni wa kupongezwa na mpenda maendeleo yeyote na kubainisha kuwa waliokuwa wamesafiri miaka ya nyuma hakuna jambo la ajabu walilofanya.

Mhadhiri Mwandamizi wa UDSM, Dk Benson Bana alisema kilichotokea ni Rais kufanya siasa, hivyo njia rahisi ya kuwaonesha wapiga kura kuwa yuko nao ni lazima atoe ujumbe aliotoa.

Alisema Rais amekuwa akizungumza kuhusu haiba ya Tanzania anayoitaka, hivyo kwa utaratibu huo anaofanya anataka kuwahakikishia kuwa yuko nao katika kupigania mahitaji yao.

“Nadhani alitaka kuonesha kuwa anabana matumizi ili kujenga Tanzania ya uchumi wa kati na katika hilo dawa ni kuzuia safari zikiwamo zake,” alisema.

Tangu Rais Magufuli achaguliwe Oktoba 25 na kuapishwa Novemba 5 mwaka juzi amekuwa nchini na alifanya ziara za Rwanda, Kenya na Uganda  jambo ambalo limekuwa likiibua maswali mengi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo