…JPM: Msiwahusishe Mkapa, JK na makinikia


Mwandishi Wetu

Rais John Magufuli
RAIS John Magufuli amevionya vyombo vya habari vinavyowataja marais wastaafu Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete vikiwahusisha na taarifa za kamati mbili za uchunguzi wa makinikia zilizokabidhiwa kwake.

Dk Magufuli alitoa onyo hilo jana, siku tatu baada ya kupokea ripoti ya Kamati ya pili aliyounda ikiongozwa na Profesa Nehemiah Osoro ambayo ilichunguza maeneo ya kisheria na kiuchumi kuhusu mikataba ya madini na mchanga wa madini.

Hata hivyo, baada ya kupokea ripoti hiyo, wadau wa masuala ya mikataba ya madini wakiwamo wanasheria na wanasiasa, wamekuwa wakihusisha mikataba hiyo mibovu ya madini na viongozi wastaafu wa awamu ya tatu na nne, Mkapa na Kikwete maelezo ambayo yamekuwa yakiripotiwa na vyombo vya habari.

Hata hivyo, Rais Magufuli amezuia wastaafu hao kutajwa akisema: “Nimesoma ripoti zote mbili hakuna mahali ambapo Mzee Mkapa na Mzee Kikwete wametajwa, vyombo vya habari viache kuwachafua hawa wazee, wamefanya kazi kubwa ya kulitumikia Taifa letu, viwaache wapumzike.”

Kauli hiyo ya Rais Magufuli imo katika taarifa yake iliyotumwa kwa vyombo vya habari ambayo baadaye ilikaziwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe.

Akikazia onyo hilo la Rais, Dk Mwakyembe alisema: “Ikumbukwe kwamba taarifa iliyotolewa na Kamati haikuwataja, wala kuwatuhumu marais hao wastaafu na Serikali ya Awamu ya Tano…, inawaheshimu na kutambua mchango wao adhimu katika kujenga ustawi wa nchi yetu.”

Aliongeza: “Naviasa vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kuacha mara moja mwelekeo huo hasi, ambao una kila dalili ya kututoa kwenye mstari na kupotosha kampeni tuliyonayo ya kujikomboa kiuchumi.”
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo