Chuo chaanzisha kozi za Shahada


Mwandishi Wetu

Waziri Joyce Ndalichako
CHUO cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kimeanzisha masomo ya Shahada ya Kwanza ya Uhazili na Utunzaji Kumbukumbu, Taarifa na Nyaraka.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Mkuu wa Chuo hicho, Dk Henry Mambo alitoa mwito kwa watumishi wa umma na Watanzania wenye sifa, kuchangamkia nafasi hizo za masomo kwa manufaa yao binafsi na Taifa.

Dk Mambo alisema masomo hayo yataanza Septemba katika matawi ya Dar es Salaam na Tabora na mengine yatafuata.

Alisema mwombaji anatakiwa kuwa na elimu ya kidato cha sita na ufaulu wa masomo mawili au Diploma katika fani husika yenye ufaulu au GPA ya alama 3.

Mkuu huyo alifafanua, kwamba masomo hayo ya ngazi ya Shahada yameanzishwa ili kuhakikisha kwamba watumishi wa umma wanaongeza elimu kwenye fani hiyo na kupanua soko la ajira.

“Kutokana na mabadiliko ya teknolojia na mifumo ya utendaji kazi ni vema watumishi wa umma na Watanzania wenye sifa, wakapata mafunzo ya kuwawezesha kukabiliana na changamoto katika soko la ajira,” alisema.

Alibainisha, kwamba mafunzo hayo yatawezesha wahitimu kutekeleza majukumu yao kwa ufasaha zaidi na hivyo kuchangia uendelezaji na ukuaji wa taaluma ya utunzaji kumbukumbu, taarifa na nyaraka.

Katibu Mkuu wa Chama cha Makatibu Mahsusi Tanzania (TAPSEA), Festo Melkiory alisema kuanzishwa kwa kozi hizo ni fursa kwa Watanzania hususan makatibu mahsusi na watunza kumbukumbu.

Alisema matumaini yake ni kuona kozi hizo zinaongeza weledi na ujuzi miongoni mwa watumishi wa umma na Watanzania.

“Hiki kilikuwa ni kilio chetu cha siku nyingi, sasa kimesikilizwa, ni matumaini yangu kuwa makatibu mahsusi wengi wataichangamkia fursa hii,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo