Tanzania kuendelea kuhudumia wakimbizi


Abubakari Akida

Wakimbizi kutoka Burundi
SERIKALI imeahidi kuendelea kutoa huduma kwa wakimbizi ikishirikiana na mashirika ya ndani na nje ya nchi, huku akiziomba nchi zenye machafuko kukaa na kutatua changamoto zinazofanya watu kukimbia nchi zao.

Ahadi hiyo ya Serikali ilitolewa juzi na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Mwinyi, alipozungumza kwenye maadhimisho ya Siku ya Wakimbizi Duniani, iliyofanyika Dar es Salaam.

Balozi Mwinyi alisema Serikali ya Tanzania imekuwa ikisaidia masuala ya wakimbizi tangu awamu ya Baba wa Taifa na Rais wa Kwanza, Mwalimu Julius Nyerere, ikiwamo kuwapa huduma za afya na elimu, ili kutimiza ndoto zao za kabla ya kukimbia nchi zao.  

“Tuunge mkono nguvu ya pamoja kuhakikisha tunamaliza migogoro kupitia njia ya mazungumzo, ili kumaliza tatizo la wakimbizi duniani, na tushirikiane na nchi zinazowahifadhi na mashirika ya kimataifa tukijua kuwa jukumu la kutatua changamoto hii ni letu,” alisema Balozi Mwinyi

Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) nchini, Alvaro Rodriguez alisema Umoja wa Mataifa kupitia Shirika lake la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) lina mkakati maalumu wa kuwahudumia na nchi zinazowahifadhi (CRRF) kwa lengo la kukabiliana na changamoto za kimaendeleo dhidi ya wakimbizi katika kambi zao.

Mwakilishi wa UNHCR nchini Tanzania, Chansa Kapaya alisema Shirika lake litaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania kuhakikisha wakimbizi wanaendelea kupokea misaada ya kibinadamu katika mazingira  yanayowaruhusu kuishi kwa usalama na hadhi.

Juni 20 dunia huadhimisha Siku ya Wakimbizi huku ikikadiriwa kuwa kila baada ya sekunde 20 mtu hukimbia nchi yake na kuacha familia, nyumba na mali kutokana na machafuko, migogoro na uhalifu dhidi ya binadamu na kundi linaloathirika zaidi ni watoto wanaokadiriwa kuwa wengi kwa idadi ya wakimbizi milioni  65.6 duniani.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo