Wananchi 5,000 wanywa maji yasiyo salama


Ibrahim Yassin, Momba

ZAIDI ya wakazi 5,000 wa vijiji vya kata na tarafa ya Kamsamba wilayani hapa wako hatarini kukumbwa na homa za mlipuko zikiwamo   za matumbo na kuhara kwa kunywa maji yasiyo salama.

Gazeti hili limefika eneo la kitongoji cha Namaimba, kijijini Namkanga na kujionea wananchi wakitumia maji machafu yenye wadudu na harufu mbaya, ambao wameomba kuondolewa kero hiyo wasiendelee kudhurika.

Wakizungumza jana kwa masikitiko, wakazi hao wa bonde la Kamsamba, walisema kwa muda mrefu sasa wamekuwa wakinywa maji machafu kutokana na ukame uliowakumba huku wakiiomba Serikali kuwaondolea changamoto hiyo.

Ernest Kaponela wa Kamsamba, alisema tangu azaliwe na sasa ana umri wa miaka 42 hawajapata maji safi na salama, zaidi ya kunywa maji machafu na kuwa endapo Serikali haijaona umuhimu huo, kuna uwezekano wa wakazi wengi kudhurika.

Ketasia Gaudence wa Kamsamba pia, alisema wao hasa watoto wao wamekuwa wakikumbwa na magonjwa ya milipuko, kutokana na kunywa maji yasiyo salama na kuwa kibaya zaidi miundombinu ya barabara ni mibovu huku zahanati iko mbali na vijiji vyao.

Alisema ili kuondokana na hali hiyo, ipo haja Serikali kwa kushirikiana na wadau, kuharakisha upatikanaji huduma ya maji safi na salama kwenye bonde hilo, ili kuokoa afya na maisha ya wakazi wa eneo hilo yasizidi kutokea.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kamsamba, Joseph Simfukwe alisema wamekuwa wakizungumzia kila mara vikaoni kuhusu upatikanaji maji kwenye bonde hilo, lakini hali bado ni tete na iwapo hatua za makusudi hazitachukuliwa, kuna uwezekano wa kutokea madhara makubwa kwa wananchi.

Diwani wa Kamsamba, Prosper Nyalali alikiri kuwapo tatizo na kuwa amekuwa akipeleka taarifa kwenye vikao vya Baraza la Madiwani, lakini hali bado ni tete licha ya kuwa tayari mpango mkakati wa Serikali umeanza kufanyika.

Mkuu wa Wilaya ya Momba, Juma Ilando naye alikiri kuwapo na changamoto hiyo hasa kwa bonde la Kamsamba na kusema ameagiza watendaji wa Halmashauri kufanya utafiti kujua idadi ya visima vya wilaya nzima, ili vilivyoharibika vitengenezwe na mahali ambako havipo wachimbe ili kuondoa tatizo hilo.

Mbunge wa Jimbo hilo, David Silinde alisema kutokana na uhaba wa maji jimboni, aliomba msaada bungeni ili kuhakikisha Serikali inaondoa tatizo hilo na tayari upembuzi yakinifu ulifanyika muda mrefu na kwamba utekelezaji wa kuondoa tatizo hilo utafanyika.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo