Rais mstaafu ahukumiwa miaka 10 jela


BRASILIA, Brazil

Luiz Inacio Lula da Silva
RAIS mstaafu Luiz Inacio Lula da Silva, amgombea urais anayepewa nafasi kubwa ya kurudi madarakani katika uchaguzi mkuu wa mwakani, amekutwa na hatia ya rushwa na kuhukumiwa kifungo cha karibu miaka 10 jela.

Uamuzi huo wa Mahakama uliotolewa juzi ni anguko kubwa kwa Lula, mmoja wa wanasiasa maarufu nchini, na pigo kubwa kwa fursa ya yeye kutaka kurejea madarakani.

Kiongozi huyo wa zamani, ambaye alisifika kwa sera zake za kupunguza pengo la utofauti wa kipato nchini, anakabiliwa bado na mashitaka mengine manne ya rushwa, lakini ataendelea kuwa huru kutokana na kukata rufaa.

Uamuzi huu unatokana na uchunguzi dhidi ya tuhuma za rushwa ambao kwa zaidi ya miaka mitatu sasa umeitikisa nchi, ukijikita katika vitendo hivyo katika ngazi za juu za jumuiya ya wafanyabiashara na Serikali.

Jaji Sergio Moro alimkuta Lula (71) na hatia ya kukubali dola milioni 1.2 kama rushwa kutoka kampuni ya uhandisi ya OAS SA, kiwango cha fedha ambacho waendesha mashitaka, walisema kampuni hiyo ilikitumia kukarabati hekali lililoko ufukweni kwa ajili ya Lula kama shukurani ya msaada wake ulioiwezesha kampuni ya Taifa ya mafuta ya Petroleo Brasileiro (PETR4.SA) kupewa ukandarasi.

Waendesha mashitaka walimtuhumu Lula, Rais wa kwanza kutoka kundi la wafanyakazi tangu mwaka 2003 hadi 2011, kusimamia mtandao wa rushwa uliogundulika hivi karibuni kutokana na uchunguzi kuhusu tuhuma zilizoigubika kampuni ya Petrobras.

Timu ya wanasheria wa Lula ilisema katika taarifa yake kupitia barua pepe, kwamba hana hatia na  itakata rufaa.

“Kwa zaidi ya miaka mitatu, Lula amekuwa akichunguzwa kisiasa,” waliandika. “Hakuna ushahidi wa maana wa kumweka hatiani uliotolewa na hata uthibitisho kwamba hana hatia ulipuuzwa.”

Wakili wa Lula, Cristiano Martins amekaririwa mara kwa mara akimtuhumu Jaji Moro kwa kulalia upande mmoja dhidi ya mteja wake, tuhuma ambazo Moro anazikanusha. 

Moro aliandika kwenye uamuzi wake kwamba “hakufikia uamuzi huo kama kujifurahisha binafsi, bali ni kinyume chake.

“Inalalamikiwa kwamba Rais wa Jamhuri amepatikana na hatia ya jinai,” Moro alisema. “Haijalishi una umuhimu gani, hakuna aliye juu ya sheria.”

Lula atazuiwa kugombea urais iwapo adhabu yake itaendelea hata baada ya kukata rufaa mahakamani, ambayo inatarajiwa kuchukua takriban miezi minane hata kutolewa uamuzi.

Asipogombea, mchambuzi wa siasa anasema Brazili itaingia kwenye msambaratiko na kulazimika kujengwa upya, na pengine kupata kiongozi ambaye anaweza kujitokeza kwenye kivuli ambacho Lula alikiweka kwenye siasa za Brazili kwa miongo mitatu.

“Kukosekana kwa Lula kunasababisha uwazi ndani ya siasa, kunaweka ombwe la madaraka,” alisema Claudio Couto, mwanasayansi ya siasa wa Wakfu wa Getulio Vargas ambacho ni Chuo Kikuu maarufu.

“Tumeingia katika mvutano mkubwa wa kisiasa, hata zaidi ya mgogoro tuliokuwa nao mwaka jana.”

Couto alisema anatarajia uamuzi huo dhidi ya Lula utasimamishwa na Mahakama ya Rufaa. Hali ambayo itafanya mbio za urais mwakani kuwa wazi na kutoa fursa ya ushindi kwa mwanasiasa kutoka nje, kutokana na wanaopewa nafasi ya kuwania, nao kuwa wamechafuliwa na tuhuma za rushwa nchini.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo