ADC: Hali ya kisiasa siyo nzuri


Abraham Ntambara

Raisi John Magufuli
CHAMA cha Alliance for Democratic Change (ADC), kimemuomba Rais John Magufuli kuachia vyama vya siasa vya upinzani kufanya shughuli za kisiasa kwa kuwa ni takwa la kisheria.

Kauli hiyo imetolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Taifa wa chama hicho, Doyo Doyo aliyesema hali ya kisiasa nchini si nzuri na kwamba Serikali kwa kuendelea kuzuia shughuli za kisiasa ni tishio kwa vyama kama ADC akisema huenda vikafa.

“Hali ya kisiasa sio nzuri sana, kuna hali ya kutopata uhuru wa kufanya siasa hasa katika upande wa vyama vya upinzani katika nchi yetu. Kuzuiwa kufanya mikutano ya kisiasa, makongamano na kadhalika, hii inaua vyama vya siasa,”alisema na kuongeza:

“ADC inamuomba Rais John Magufuli atuachie tufanye mikutano kwani jambo hili ni takwa la kisheria.”

Akizungumzia usalama nchini alisema hawaridhishwi na taarifa za mauaji yanayoendelea Kibiti mkoani Pwani akisema yanatia doa Taifa, ambapo aliiomba Serikali kujipanga upya na kuweka mkakati madhubuti ya kukabiliana na wahalifu.

Kuhusu migogoro ndani ya vyama vya siasa Doyo alisema ADC kinashangazwa na mgogoro wa Chama cha Wananchi (CUF) kushindwa kupatiwa ufumbuzi wa haraka hali inayofanya wanachama wake kuanza kukata tamaa.

Alisema ADC unachukizwa na hali hiyo kwani kuendelea kwa mgogoro huo kwa muda mrefu ni kunadhoofisha afya ya upinzani katika macho ya Watanzania.

“Nawaomba Maalim Seif Sharif Hamad na Profesa Ibrahim Lipumba wakae pamoja ili kumaliza tofauti zao,” alisema Doyo.

Aidha, alieleza kushtushwa kwa ADC na matamko mbalimbali ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuingilia mgogoro huo wa CUF.

Doyo aliwashauri Chadema kuacha mara moja kuingilia mgogoro usiowahusu akidai kitendo hicho cha kuingilia mgogoro huo usiowahusu ni mkakati wa kisiasa wa kujitengenezea hati miliki ya kisiasa nchini, lakini pia kinaweza kuhatarisha amani.

Hata hivyo, Doyo alisema alimpongeza Rais Magufuli kwa juhudi zake anazofanya kuzuia rasilimali za nchi hasa kwa kitendo cha kuwasilisha miswada kwa hati ya dharura bungeni ili kufanyiwa marekebisho ya sheria.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo