Luoga ateuliwa Mwenyekiti Bodi ya TRA


Suleiman Msuya

Dk.John Magufuli
RAIS John Magufuli amemteua Profesa Florens Luoga kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Profesa Luoga anachukua nafasi ya Bernard Mchomvu ambaye Bodi yake ilivunjwa na uteuzi wake kutenguliwa Novemba 20 mwaka jana na Rais Magufuli.

Luoga ameteuliwa kushika nafasi hiyo akitokea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ambako ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho Taaluma.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu, uteuzi wa Profesa Luoga ulianza jana.

Uvunjwaji wa Bodi ya awali ulitangazwa na Rais Magufuli wakati akiongoza Mahafali ya 31 ya Chuo Kikuu Huria yaliyofanyika Kibaha, Pwani ambako alisema Bodi hiyo iliidhinisha Sh bilioni 6 zilizotengwa kwa matumizi ya TRA kupelekwa kwenye benki kwenye akaunti ya muda maalumu.

“Bodi imepitisha fedha kwenda kwenye akaunti ya muda maalumu kinyume na maagizo ya Serikali, ndiyo maana nilipozipata hizo fedha nimezichukua na Bodi kwa heri,” alisema.

“Kumekuwa na mchezo huu kwa wakurugenzi watendaji wengi zinapotolewa fedha kwa  ajili ya kwenda kwenye miradi fulani, zile fedha wanazochukua wanaziweka kwenye benki za biashara, na kuweka akaunti maalumu kwa mazungumzo ya uelewano kati ya huyo mkuu wa taasisi na benki husika. Waziri hiyo message sent and delivered,” alisisitiza.

Wasifu

Profesa Luoga alizaliwa mwaka 1958 na mwaka 1985 alipata Shahada ya Kwanza ya Sheria katika Chuo Kikuu cha UDSM, mwaka 1988 alihitimu Shahada ya Pili ya Uzamili ya Chuo Kikuu cha Queen’s cha Canada na mwaka 1991 alihitimu Shahada ya Uzamili katika Sheria za Kimataifa kwenye Chuo cha Lund, Sweden.

Mwaka 2003 alitunukiwa Shahada ya Uzamivu kwenye Chuo Kikuu cha Warwick cha Uingereza.

Aidha, mwaka 1986, Profesa Luoga aliajiriwa UDSM katika Kitivo cha Sheria kama Mhadhiri Msaidizi ambapo mwaka 2005 alipandishwa kuwa profesa.

Pia alishika nafasi mbalimbali za utawala chuoni hapo kama Mwenyekiti Kamati ya Msaada wa Kisheria katika Kitivo cha Sheria kuanzia mwaka 1993 hadi 1995.

Profesa Luoga alipandishwa kuwa Mkuu wa Utawala Kitivo cha Sheria mwaka 1992 hadi 1995, Mkurugenzi wa Shahada ya Kwanza mwaka 2005 hadi 2009, Kaimu Naibu Mkuu wa Chuo Taaluma mwaka 2013 hadi sasa na pia ni Wakili wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Hali kadhalika Profesa Luoga ametoa machapisho mbalimbali kuhusu kodi, haki za binadamu, sheria na manunuzi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo