Jitihada za Samia kwenye afya zazaa matunda


Mwandishi Wetu

Makamu wa Rais, Samia Hassan Suluhu
JITIHADA za Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan kusaidia uboreshaji huduma za afya hasa kwa wanawake nchini, zimeendelea kuzaa matunda.

Hiyo inatokana na taasisi ya Merck yenye makao yake nchini Ujerumani kumwahidi kuanzisha mpango wa kugharimia mafunzo maalumu kwa wataalamu wa afya nchini, hasa ya saratani kwa watoto, matibabu yake kwa upasuaji na utabibu kwa Tanzania Bara na Zanzibar.

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Merck, Dk Rasha Kelej ametoa kauli hiyo baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais, Ikulu, Dar es Salaam, ambako alisema taasisi hiyo imejitolea kuisaidia Serikali kuboresha sekta ya afya kupitia mpango huo unaotarajiwa kuanzishwa mwishoni mwa mwaka huu.

Dk Kelej alisema mafunzo hayo kwa wataalamu wa afya yatatolewa kati ya mwaka mmoja hadi mitatu India, Ulaya na Kenya kwa lengo la kuboresha upatikanaji huduma zote kuhusu saratani nchini.

Taasisi ya Merck pia ilimhakikishia Makamu wa Rais kuwa itajikita kuwajengea uwezo wanawake wenye matatizo ya ugumba kwa kuhakikisha wanapata taarifa sahihi kuhusu matatizo ya ugumba, hivyo itasaidia kubadilisha mtazamo uliojengeka kwenye jamii kuhusu   ugumba kwa wanawake.

Ajenda hiyo itasimamiwa kupitia programu ya Merck More Than a Mother.

Kwa mujibu wa takwimu za watendaji wa taasisi hiyo, tatizo la ugumba kwa wanandoa Afrika ni kubwa na inakadiriwa kwamba katika kila ndoa nne, moja inasumbuliwa na ugumba na karibu asilimia 85 ya ugumba inasababishwa na ukosefu wa matibabu kwa magonjwa yanayoweza kutibika.

Aidha, Makamu wa Rais aliipongeza taasisi ya Merck kwa juhudi zake za kuboresha sekta ya afya Afrika na aliikaribisha kufanya kazi nchini.

Samia alifurahishwa na mipango na mikakati ya taasisi hiyo na kwamba Serikali iko tayari kushirikiana nayo kuwajengea uwezo kina mama na utoaji mafunzo kwa wataalamu wa sekta ya afya nchini hasa kwenye saratani na ugumba.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo