Serikali kukusanya milioni 300/- za Nanenane


Venance Matinya, Mbeya

Jiji la Mbeya
SIKU chache baada ya Chama cha Wakulima Tanzania (TASO) kufutiwa usajili na kuzuiwa kujihusisha na makusanyo ya fedha kwa maandalizi ya Maonesho ya Wakulima (Nanenane) mwaka huu, Serikali imejipanga kukusanya zaidi ya Sh milioni 300 kupitia vyanzo vyake. 

Akitoa juzi taarifa ya maandalizi ya maonesho na sherehe za Nanenane mwaka huu Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, kwa niaba ya Sekretarieti ya Kanda, Katibu Tawala Msaidizi wa Uchumi na Uzalishaji wa Mkoa, Nyasebwa Chimagu alisema matarajio ni kukusanya Sh 335,543,801. 

Alisema makusanyo hayo yanatarajiwa kutokana na vyanzo mbalimbali vikiwamo vya ofisi za mkoa, halmashauri, tozo na ada za ushiriki kutoka mashirika na taasisi za umma na binafsi. 

Aliongeza kuwa kati ya hizo, Sh 138,443,801 zitatoka sekretarieti za mikoa na halmashauri, huku Sh 197,100,000 zikitokana na vyanzo vingine kama ada za ushiriki, tozo za viwanja, viingilio na ushuru uwanjani. 

Chimagu alisema hali ya makusanyo hadi Julai 6 hairidhishi, kwani ni Sh milioni 35 tu zilizokusanywa kutoka baadhi ya sekretarieti za mikoa na Halmashauri. 

Kwa hali hiyo, Mwenyekiti wa Kikao hicho ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa, Amos Makalla aliagiza halmashauri na mikoa yote kuhakikisha inamaliza kutoa michango yao hadi Julai 15.

Alisema ili kukamilisha maandalizi ya maonesho, kinachotakiwa ni fedha hivyo ni vema halmashauri zikajipanga mapema kuruhusu sekretarieti kuandaa sherehe vizuri. 

Wakuu wa Mikoa ya Njombe na Ruvuma, Christopher ole Sendeka na Dk Binilith Mahenge walisisitiza washiriki kutoa michango yao mapema ili kufanya maandalizi mapema ikiwa ni pamoja na kujiandaa na maonesho ya kimataifa. 

Walisema endapo hadi Julai 15 kutakuwa na halmashauri isiyomaliza madeni yake, itazuiwa kushiriki maonesho ya Nanenane mwaka huu.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo