Lowassa apigwa kalenda tena na DCI


Grace Gurisha

Edward Lowassa
WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, ameripoti kwa mara ya tatu Makao Makuu ya Jeshi la Polisi kama alivyoelekezwa na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).

Huo ni mwendelezo mahojiano yake na Polisi baada ya hivi karibuni kudaiwa kutoa kauli za uchochezi.

Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Chadema alifikia kwa DCI jana saa tatu asubuhi akifuatana na baadhi ya wanasheria wa chama hicho, lakini baada ya mahojiano mafupi alitoka, huku taarifa kutoka ofisi ya DCI ikieleza kuwa Lowassa anatakiwa kuripoti tena Julai 20.

Lowassa anadaiwa kutoa kauli za uchochezi kwenye futari iliyoandaliwa Juni 23 na Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara na baada ya kauli yake hiyo, alipokea mwito wa DCI ambako alihojiwa kwa saa nne kabla ya kutakiwa kuripoti tena Juni 29.

Katika futari hiyo, Lowassa anadaiwa kutoa maneno ya uchochezi kuhusu mashehe wa taasisi ya Uamsho wanaoshikiliwa na magereza, akitaka utaratibu wa kisheria utumike kuwaachia huru mashehe hao.

Mara ya pili alipofika kwa DCI alitakiwa kurudi tena jana, huku kauli ya Rais John Magufuli ya kulitaka Jeshi la Polisi kukamata watu wote wanaozungumzia mashehe hao na kuwahusisha na mauaji yanayoendelea mkoani Pwani, ikitafsiriwa kuwa huenda hali ingekuwa mbaya zaidi kwa Lowassa.

Hata hivyo, jana hali ilikuwa tofauti huku wakili wake, Peter Kibatala akisema mbunge huyo wa zamani wa Monduli alitekeleza agizo hilo kama alivyoelekeza, kuripoti tena Julai 20, saa 3 asubuhi.
Alisema sababu kubwa waliyoeleza ni kwamba upelelezi haujakamilika na kubainisha kuwa Lowassa hakukaa kwa muda mrefu kabla ya kuruhusiwa kuondoka.

“Upelelezi bado haujakamilika ametakiwa kurejea tena Polisi Julai 20,” alisema Kibatala.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo