Wasira aomba suluhu Chadema, Serikali



* Asema JPM asiachwe aingie vitani na wapinzani, Lowassa msingi wa maandamo

Suleiman Msuya na Mashaka Mgeta

KADA mwandamizi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Steven Wasira amesema wasaidizi wa Rais John Magufuli, hawapaswi kumuacha kiongozi huyo aingie vitani dhidi ya wapinzani waliotangaza kufanya maandamano na mikutano nchi nzima kuanzia Septemba Mosi mwaka huu.

Wasira ambaye pia aliwahi kuwa mwanachama wa Chama cha NCCR-Mageuzi pamoja na kushika nafasi mbalimbali za uwaziri tangu Serikali ya awamu wa kwanza na ubunge wa Bunda kwa vipindi tofauti, alisema ipo haja ya kuwapo mazungumzo kati ya pande mbili zinazohusika ili kufikia muafaka na kwamba nafasi hiyo ipo.

“Kinachohitajika ni wasaidizi wa Rais kumshauri ili kuhakikisha kuwa tofauti zilizopo baina yake na vyama vya upinzani haziendelei ili kuepusha madhara yanayoweza kuzuilika, itafutwe suluhu,” alisema Wasira.

Aliongeza: “Wazungumze, wasimuingize Rais kupigana na watu wake kwa maana wote tutapoteza. Kwa nini uweke askari polisi wote hao, msimweke Rais kwenye vita.”

Maandamano hayo yaliyoandaliwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kupewa jina la Umoja wa Kupambana na Udikteta Tanzania (Ukuta), yameibua taharuki kwa umma na malumbano kati ya Chadema na watawala.

Viongozi wa serikali akiwamo Rais Magufuli na makamanda wa jeshi la polisi, wamekaririwa mara kadhaa wakionya kuwashughulikia washiriki wa maandano na mikutano hiyo, huku Chadema ikijinadi kuwa maandalizi yao yanakwenda vizuri.

Kauli hiyo ya Wasira imekuja wakati juzi na jana mitandao ya kijamii na vyombo kadhaa vya habari, vilichapisha picha za askari wenye sare, wengine wakiwa na silaha wakifanya doria barabarani kwa kile kilichoelezwa kuwa ni mazoezi ya kukabiliana na uhalifu na wahalifu.

Alisema ni wakati mwafaka kwa Bunge kupitia Spika Job Ndugai, kuwakutanisha wapinzani, serikali na kutoa ushauri unaofaa kwa rais Magufuli ili kuepusha hali hiyo kwani hakuna sababu ya nchi kuingia katika malumbano yasiyokuwa na tija.

Kwa mujibu wa Wasira, Bunge ni chombo kinachovikutanisha vyama vyenye wabunge hivyo kuwa sehemu muafaka kwa mazungumzo yenye lengo la kuleta muafaka huku yakisimamiwa na Ndugai aliyeonesha kutoridhishwa na hali ilivyo sasa.

“Nadhani wangelitumia Bunge kutoa kero zao ili kuhakikisha Serikali inazifanyia kazi, hivyo kuepuka kasumba ya kutoka bungeni,” alisema.

Alisema kitendo cha upinzani kujiandaa kufanya mikutano na maandamano inaweza  kuibua mambo ambayo hayakutarajiwa hivyo Serikali inapaswa kuangalia kabla ya kuruhusu.

TATIZO NI LOWASSA

Wasira alisema msingi wa kuzuiwa mikutano na maandano ya wapinzani inawezekana ikawa ni kumzuia aliyekuwa mgombea urais mwaka 2015 kupitia Chadema, Edward Lowassa, asifanye ziara ya nchi kuwashukuru waliompigia kura.

"Wakati wa uchaguzi nchi inachemka kwa harakati ambazo zinafanyika hivyo ukiruhusu mikutano kwa muda mchache baada ya uchaguzi unaweza kurejesha hali ambayo inaweza kuongeza migongano," alisema.

Alisema azma hiyo ya upinzani ingeweza kurejesha hisia za umma kwenye uchaguzi uliopita hivyo kuathiri mipango ya Rais Magufuli katika kuwatumikia wananchi kupitia kauli mbiu ya ‘Hapa kazi tu’.

Alisema baada ya uchaguzi kumalizika, Lowassa, alitangaza kushinda kwa asilimia 62, hivyo akiachwa kutoa shukrani nchi nzima, anaweza kusababisha migongano, hivyo si vema kuruhusu mikutano kwa sasa.

“Hebu fikiria kama wananchi watatangaziwa kuwa Lowassa atakuwa katika maeneo yao, kuna uwezekano wa shughuli kusimama kwani ni mtu ambaye alifanikiwa kupata kura nyingi katika historia ya uchaguzi hapa nchini,” alisema.

Aliongeza, “ukiwaruhusu kufanya mikutano na ukawaambia kuwa atakayekuja kutoa shukurani ni Lowassa, ambaye amekuwa akipinga kushindwa ni sawa na kurejesha hali ya uchaguzi kipindi hiki.”

 Wasira aliwataka viongozi wa serikali wasiishie kutoa matamko ya kupiga marufuku maandamano na mikutano ya Chadema, bali waelezee sababu ili kutoa elimu pana kwa jamii.

“Kama mimi hapa nimetaja sababu kwamba inaweza kuwa ni Lowassa, sasa na wao (serikali) wasiseme tu tunapiga marufuku mikutano na maandamo, wataje na kuzifafanua sababu za kufanya hivyo ili kuepusha upotoshaji,” alisema.

AWASAA CHADEMA

Hata hivyo Wasira alisema demokrasia na uhuru ni mambo mazuri lakini yana mipaka hata kama yatatokana na Katiba ya nchi.

Kwa hali hiyo, aliiasa Chadema kuondokana na siasa za maandamano na mikutano baada ya Uchaguzi Mkuu, kama ilivyo kwa mataifa makubwa kama Marekani, Uingereza na Ujerumani.

“Hakuna demokrasia na uhuru isiyo na mipaka, nataka nikuambie ukweli katika dunia yote uhuru wa mikutano na maandamano umeandikwa katika Katiba zao ila lazima kufuata taratibu," alisema.

Wasira alisema kumbukumbu zake ni kwamba Chadema imekuwa ikifanya mikutano kila baada ya uchaguzi jambo ambalo linaonekana kuwa ni mkakati wa kukwamisha Serikali isifanye kazi zake ipasavyo.

Wasira alisema mitizamo na utashi wa kuongoza nchi vinatofautiana kati ya viongozi, hivyo akawataka Chadema wasitarajie mfumo wa uongozi wa Rais Magufuli uwe sawa na Rais msraafu Jakaya Kikwete.

“Kikwete alikuwa anawaita Ikulu tunazungumza, tunakula chakula pamoja, hivyo wasifikiri kwamba Rais Maufuli naye atakuwa hivyo…wanapaswa kuyasoma mazingira yaliyopo sasa ingawa Katiba na sheria zinaruhusu yanayosimamiwa na serikali,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo