IGP asubiri barua ya Ukuta wa Chadema




Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe
WAKATI Chadema ikitangaza msimamo wa kuzindua Operesheni ya Umoja wa Kupambana na Udikteta Tanzania (Ukuta) Septemba mosi, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Ernest Mangu amesema hajapata taarifa kuhusu suala hilo na hivyo hawezi kulizungumzia.

Akizungumza na Jambo Leo jana, Mangu alisema kama angekuwa amepelekewa barua kuhusu mchakato huo angezungumza, lakini kutokana na kuwa suala hilo bado halijafanyika hawezi kuzungumza.

"Siwezi kuzungumza chochote kuhusu hilo, kwa maana hawajaleta barua yoyote ya kujulisha kuwa siku hiyo watafanya maandamano na mikutano nchi nzima," alisema Mkuu wa Polisi.

Alitaka aachwe hadi chama hicho kitakapopeleka barua ndipo atoe majibu kuwa ni hatua gani zitachukuliwa. "Subirini niletewe barua kueleza kuwa wanataka kufanya nini na baada ya hapo nitatoa majibu, maana kwa sasa nitakuwa nazungumza wakati barua sijaiona," alisema.

Chadema

Chadema ilisema msimamo wake kuhusu kuandamana na kufanya mikutano kuanzia Septemba mosi uko palepale kwani lengo lao ni kulinda Katiba na sheria za nchi.

Aidha, ilisema maandamano yao yatakuwa ya amani, hawatavunja sheria za nchi na kuwa lengo la kufanya hivyo ni kupigania haki za Watanzania wengi ambao wanakosa haki zao.

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Salim Mwalimu wakati akizungumza na gazeti hili jana, alisisitiza kuwa wako tayari kwa mazungumzo iwapo watahitajika kabla ya tukio hilo. Mwalimu alisema tafsiri ya Ukuta, si kufanya fujo bali kupinga mfumo wa uongozi wanaodai kuwa umekuwa wa mtu mmoja.

Alisema Chadema kupitia kamati ndogo ambazo ziliundwa, inaendelea na maandalizi ya mikutano na maandamano nchi nzima Septemba mosi na kutaka wanachama na Watanzania kuhakikisha wanatekeleza azimio hilo kwa amani na utulivu.

"Chadema hatuna ugomvi na Jeshi la Polisi na hatutarajii kupambana nao tunachotaka ni kuonesha kuwa hatukubaliani na uamuzi ambao Serikali kupitia Rais John Magufuli aliutoa wa kuzuia mikutano hadi mwaka 2020," alisema.

Mwalimu alisema haiwezekani wakakubaliana na hali hiyo, kwani siasa ndiyo kazi iliyomfanya awe Chadema na kuacha ajira zingine ambazo zilikuwa zinamtaka akae ofisini.

Alisema jambo la kusikitisha ni kuona Rais anafanya mikutano na kutumia nafasi hiyo kuwakebehi, jambo ambalo si la kiungwana na eneo sahihi la kujibu hoja zake ni kupitia mikutano kama anavyofanya yeye.

"Tunafuatilia kila anachofanya kwenye mikutano yake, hazungumzii Serikali yake ila muda mwingi anatusema sisi na kupandisha jukwaani watu wake, ili kutusema hii haikubaliki, hivyo tutapigania haki hii ya kufanya mikutano bila kurudi nyuma," alisema.

Aidha, Mwalimu alivitaka vyama vya siasa viliovyo tayari kushirikiana nao katika harakati hizo vinakaribishwa, kwani harakati hizo si za Chadema ila ni kwa faida ya Taifa. Kwa upande mwingine, Mwalimu amelalamikia Jeshi la Polisi Mkoa wa Lindi kuingia katika vikao vya ndani vya Chadema na kuchukua viongozi wao bila sababu za msingi.

Alisema kinachoonekana ni dhahiri kuwa ipo mikakati ya makusudi ya kunyanyasa wafuasi na viongozi wa Chadema, ili washindwe kufanya kazi zao kwa uhuru.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo