Viongozi wa dini waingilia kati Ukuta

VIONGOZI wa dini wameonya kwamba mvutano unaoendelea baina ya Serikali na Chadema, kuhusu Operesheni Ukuta, unaweza kuleta athari mbaya kwa Taifa, kusipofanyika mkutano wa kusaka maridhiano.

Aidha, wamesema wako kwenye mchakato wa kuandaa kikao cha dharura baina ya viongozi wa pande hizo mbili, ili kutafuta mwafaka wa kudumu kuhusu mvutano huo unaoweza kuhatarisha amani.

Katibu Mkuu wa Taasisi ya Maridhiano Tanzania, inayounda umoja wa madhehebu ya dini za kikristo na kiislamu, Mchungaji Osward Mlay alitoa tamko hilo Dar es Salaam jana kwenye mkutano na wanahabari.

Alisema wanakusudia kusuluhisha pande hizo ili kuondoa hali iliyopo bila nchi kuingia kwenye mvutano na msuguano usiokuwa na maslahi kwa Taifa.

“Tunaomba viongozi wa kisiasa na Serikali watambue sisi viongozi wa dini na taasisi ya maridhiano Tanzania tunatambua kwamba nchi yetu ni ya uongozi wa kidemokrasia na utawala wa kisheria,” alisema Mlay na kuongeza:

“Hivyo, tunaomba ninyi viongozi wetu wa kisiasa na Serikali muheshimu Katiba na sheria tulizojiwekea kama Taifa kuhusu muundo wa uongozi tunaotaka uongoze nchi yetu,” alisema.

Alihadharisha kwamba iwapo Chadema itafanya maandamano waliyopanga yanaweza kusababisha madhara kama yaliyotokea siku za karibuni Ethiopia ambako wapinzani waliingia mitaani kudai haki ya demokrasia kwa maandamano na kupambana na Dola, ambapo watu wengi waliuawa na wengine kujeruhiwa hivyo kubaki na msiba wa kitaifa.

Alionya kuwa iwapo Serikali itafanya ukandamizaji na kuminya demokrasia kama ilivyotokea Burundi kwa kutumia ubabe na mabavu ya Dola, inaweza kusababisha nchi kuingia katika machafuko na umwagaji damu za watu wasio na hatia.

Mchungaji Mlay alisema inapotokea mivutano ya namna hiyo kwenye Taifa, waathirika huwa si viongozi bali wananchi wa kawaida hasa wanawake, watoto na wazee ambao hukosa walezi ambao hupoteza maisha kwenye maandamano hayo.

“Inapotokea mivutano ya namna hii husababisha vifo, ulemavu, wajane, yatima na wazee kukosa walezi,” alitanabaisha.

Alisema viongozi wanapaswa kutambua dhamana kubwa waliyonayo kwa wananchi wanaoongoza na kutaka wawe makini wanapotoa matamko na misimamo inayosababisha kutoelewana baina yao na wananchi wa kawaida.

“Mwito wa viongozi wa dini kwa wananchi, tuilinde amani yetu tuliyoipata tangu uhuru, wananchi wa Tanzania hatuhitaji Kamati ya Umoja wa Mataifa ije kusimamia Amani tuliyonayo, sisi wenyewe tuna wajibu wa kuilinda,” alisema.

Mchungaji Mlay alibainisha kwamba jukumu walilonalo Watanzania sasa ni kusonga mbele kwa kuhakikisha wanafanya kazi za kuchochea elimu bora, kazi za kijamii, kisiasa, kiuchumi na afya, pamoja na kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji, mauaji ya albino na vikongwe, kuzuia vijana kujiingiza katika vitendo vya ukahaba na uasherati.

Pamoja na Mchungaji Mlay, mwakilishi wa Kanisa la Assemblies of God (TAG), wengine waliokuwa kwenye mkutano huo ni Shekhe Salim Juma, Shekhe Bakari Mkomeni, Askofu Msaidizi wa Kanisa la Evangelical Assemblies of God Tanzania (EAGT) na Naibu Katibu wa Taasisi ya Maridhiano na Padri Meshack Chidundwa wa Kanisa la Anglikana.

Katika siku za karibuni, kumekuwapo na mvutano kati ya Serikali kupitia Jeshi la Polisi na Chadema kuhusu kuwepo au kutokuwepo kwa mikutano ya hadhara ya kisiasa na maandamano.

Wakati Serikali ikizuia mikutano na maandamano, Chadema inadai ni haki yao kikatiba na kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa kufanya mikutano na maandamano nchi nzima Septemba mosi, kupinga wanachodai ni kuminywa kwa demokrasia kunakofanywa na Serikali.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo