Lowassa, Mbowe watiwa mbaroni



*Watuhumiwa kufanya mkutano wa ndani
*Wamo pia Mashinji, Mnyika na Said Issa

Suleiman Msuya

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limewakamata na kuwaweka mahabusu na kuwahoji viongozi waandamizi wa Chadema kwa madai ya  kufanya mkutano wa ndani bila kibali.

Taarifa zilizolifikia JAMBO LEO jana zilieleza kuwa viongozi waliokamatwa baada ya mkutano wa Kamati Kuu ya Chama hicho na kupelekwa Kituo Kikuu cha Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kwa mahojiano ni Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe, Mjumbe wa Kamati Kuu, Edward Lowassa, Katibu Mkuu, Vincent Mashinji, Naibu Katibu Mkuu Bara, John Mnyika na Makamu Mwenyekiti, Said Issa Mohammed.

Habari zaidi zilieleza kuwa viongozi hao walifanya vikao vya kawaida vya Kamati ya Kuu ili kujadili masuala ya chama ikiwamo mipango ya Operesheni ya Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania (Ukuta).

“Baada ya mkutano wa Kamati Kuu, ulianza mkutano wa wajumbe takriban 178 na ulipoanza kujadili Ukuta, polisi walivamia na kukamata viongozi wetu,” alisema mmoja wa wabunge aliyekuwa kwenye mkutano huo.

Taarifa zaidi zilionesha kuwa viongozi hao walikamatwa saa 8 mchana na kufikishwa Polisi saa 10:30 jioni.

Akizungumza na wanahabari baada ya kufikishwa   Polisi, huku Mbowe, Lowassa, Mashinji na Mnyika wakiwa ndani kwa mahojiano, Mwanasheria wa Chama hicho, Tundu Lissu alisema:

“Kamati Kuu ilianza mkutano saa 6 mchana na ikamaliza, wakati mkutano unaoshirikisha wote ulipoanza, ndipo walikuja askari  wanane waliovalia kiraia na kuwakamata.”

Hata hivyo, Lissu alisisitiza kwamba mbali na hatua hiyo ya Polisi, Chadema haitarudi nyuma huku akieleza kuwa Operesheni Ukuta iko pale pale.

“Hatutafanya kazi kwa maagizo ya mtu bali kwa kufuata sheria na Katiba ya nchi,” alisema Lissu.

Gazeti hili lilishuhudia viongozi mbalimbali na mashabiki wa Chadema wakijikusanya kwa vikundi katika viunga vya Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam na ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) jirani na kituo hicho, wakifuatilia kukamatwa kwa viongozi wao.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo