Watakiwa kuchangamkia fursa China


Salha Mohamed

Godfrey Simbeye
WATANZANIA wametakiwa kuchangamkia fursa ya maonesho ya viwanda China ili kutimiza azma ya kuwa na Tanzania ya Viwanda.

Maonesho hayo yanatarajia kufanyika Aprili 13 hadi 21 nchini humo yakitazamiwa kuleta mabadiliko katika sekta ya viwanda.

Mkurugenzi Mtendaji wa Sekta Binafsi (TPSF), Godfrey Simbeye, akizungumza jana na wafanyabiashara 20 wanaotarajiwa kwenye maonesho hayo, alisema Serikali peke yake haiwezi kuleta mabadiliko ya sekta ya viwanda.

Alisema sekta binafsi zina nafasi kubwa kuleta na kutimiza Tanzania ya viwanda, hivyo zinapaswa kutumia fursa hiyo.

"Azma ya Tanzania ya viwanda 2025 hatuwezi kuifanya tukikaa humu ndani, lazima tutoke tukaone mifano tukajifunze kwa wenzetu waliotangulia," alisema.

Alisema haiwezekani nchi kuwa na viwanda bhila kuona nchi zingine zinavyofanya huku akibainisha kuwa hata wakazi wa China walijifunza kutoka Marekani na Israel.
"Serikali pekee inatakiwa kutuwezesha kwenye miundombinu, umeme wa kutosha ujuzi wa kutosha na mambo ya kodi yanayovutia uwekezaji," alisema.

Simbeye alitoa mwito kwa wananchi kujitokeza kushiriki maonesho hayo kwani ni fursa muhimu ambayo hupatikana kila mwaka.

"Niwapongeze Watanzania wanaokwenda, kwani wamefanya uamuzi wa kuisaidia nchi, kwani kila Mtanzania ana nafasi ya kuchangia uchumi wa nchi hii," alisema.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Usafirishaji ya Kinyago Travel & Tour, Diana Gasper alisema wafanyabiashara kwenda China ni fursa kubwa katika kufanikisha azma ya Tanzania ya Viwanda.

"Ninaona fursa kubwa sana kwa Tanzania ya Viwanda, tunaposema Tanzania ya Viwanda, inaanza na mimi na wewe, hivyo ukisubiri wenzio wameanza halafu wewe ufuate, ujue wenzio tunakwenda tunakimbia," alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo