Wabunge wapinga amri za maDC, maRC


Fidelis Butahe, Dodoma

AMRI za baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya nchini kutaka Jeshi la Polisi kukamata watendaji wa Serikali, wanahabari na watu wa kada mbalimbali na kuwasweka rumande kwa madai ya kufanya makosa, zimepingwa na wabunge.

Wabunghe hao walifikia hatua hiyo jana kwa maelezo kuwa ni ukiukwaji wa sheria za utumishi wa umma na utawala bora.

Bila kujali itikadi zao, wabunge hao walisema utawala bora ni nguzo muhimu katika ujenzi wa jamii yenye umoja, usawa, mshikamano, audilifu na uwajibikaji na kuwataka wateule hao wa Rais kuacha kujigeuza miungu watu.

Wabunge walitoa kauli hiyo kwenye mjadala wa taarifa ya Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, ambayo ilitoa mifano ya amri za wakuu hao wa mikoa na wilaya licha ya kutowajata majina, huku ikisisitiza kuwa wanachokifanya si sahihi.

Akiwasilisha taarifa ya Kamati hiyo ya mwaka 2016/17, mjumbe wa Kamati hiyo Esther Mahawe alisema siku za hivi karibuni watendaji wa Serikali wamechukua nafasi ya mhimili wa Mahakama kwa kuhukumu na kuwatia hatiani baadhi ya watumishi wa umma.

“Wanafanya hivyo bila kujua, kwamba wanakiuka msingi wa Katiba waliyoapa kuilinda. Ibara ya 13 (6) na (2) ya Katiba inazuia mtu anayeshitakiwa kwa kosa la jinai, kutendwa kama mwenye kosa hilo hadi itakapothibitishwa na Mahakama yenye mamlaka,” alisema.

“Kwa hiyo, hatua ya Mkurugenzi wa Halmashauri kumwamuru mwalimu wa sekondari adeki darasa mbele ya wanafunzi wake, au Mkuu wa Mkoa kutumia lugha zisizofaa kwa watendaji ni kuwadhalilisha na kuvunja misingi ya Katiba,” aliongeza.

Mahawe alisema wateule hao wamekuwa wakitumia vibaya mamlaka waliyopewa kuamrisha watumishi wa umma kuwekwa ndani kwa makosa yasiyostahili adhabu hiyo.

“Ipo mifano kadhaa ikiwa ni pamoja na Mkuu wa Mkoa mmojawapo nchini kuamuru Daktari wa Mkoa awekwe rumande kwa sababu hakutangaza kuwapo kipindupindu,” alisema.

Alisema Mkuu wa Wilaya moja mkoani Dar es Salaam aliamuru watumishi waliochelewa kazini wawekwe ndani huku Mkuu wa Wilaya moja Arusha akiamuru mwandishi wa habari wa kituo cha televisheni awekwe ndani kwa kuandika habari kuhusu kero za ukosefu wa maji, ikidaiwa ni uchochezi.

“Sheria ya Tawala za Mikoa ya mwaka 1997 imeweka masharti muhimu kwa Mkuu wa Mkoa au Wilaya ikiwa atahitaji kutumia mamlaka ya kuamuru mtu akamatwe,” alisema.

Alibainisha kuwa vifungu hivyo vinaeleza, kwamba atafanya hivyo pale tu atakapokuwa amejihakikishia kuwa kosa lililotendwa na mhusika athari zake huwa ni kukamatwa na kushitakiwa.

 “Kamati inatambua juhudi za Serikali kurejesha nidhamu ya uwajibikaji katika utumishi wa umma…kamwe haiwezi kutetea watumishi wazembe, hata hivyo watumishi wazembe na wasiotekeleza majukumu yao wachukuliwe hatua za kinidhamu na kiuwajibikaji kwa mujibu wa taratibu zilizopo,” alisema.

Wachachamaa

Mbunge wa Muheza (CCM), Adadi Rajabu alisema wakuu hao wa mikoa na wilaya wanatumia madaraka yao vibaya na kubainisha kuwa hilo ni tatizo la kukosa semina elekezi baada ya kuteuliwa na Rais.

“Wakibishana na mtu kwenye kikao wanaamuru awekwe ndani, huo si utaratibu kabisa, kwa sababu hata polisi wanapata kozi ya miezi sita kufundishwa namna ya kukamata watu. Suala hili liangaliwe, litaleta shida,” alisema.

Mbunge wa Nzega (CCM), Hussein Bashe alisema wateule hao wa Rais katika baadhi ya maeneo ni kero kutokana na kukosa ushirikiano wa kutosha kwa viongozi wengine jambo linaloleta mgongano wa utendaji.

“Wanatakiwa kusoma sheria kabla ya kuchukua hatua kwa wananchi. Wanatakiwa kujua ni wakati gani wanakuwa na mamlaka ya kutoa amri ya kukamata mtu,” alisema Richard Mbogo (Nsimbo-CCM).

Kwa upande wake Juma Nkamia (Nchemba -CCM) alisema wamekuwa wakitoa kauli zisizofaa kwa viongozi wa maeneo yao na kuibua mgawanyiko.

 Mbunge wa Ukonga (Chadema), Mwita Waitara alisema wakuu hao wa mikoa na wilaya wamejivika kofia ya utais katika maeneo yao ya kazi jambo ambalo si sahihi.

“Wanatoa amri za vitisho kwa kweli ingawa mimi namtambua Rais mmoja tu, John Magufuli,” alisisitiza Waitara.

Awali, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-Tamisemi, George Simbachawene alisema, “"Ni kweli wapo baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya wanakiuka utaratibu wa kazi, lakini tufahamu kuwa wao ni binadamu. Kama kuna kiongozi anakwenda kinyume na sheria ni suala la mawasiliano tu arekebishwe.”

Pia, alisisitiza kuwa wana mamlaka kisheria kupewa ulinzi wa askari saba hadi 11 kwa mujibu wa sheria.

Baadhi ya matukio
Aprili 7 mwaka jana, mkuu wa Wilaya ya Chato, Shaaban Ntarambe alimuweka mahabusu mwandishi wa gazeti moja la kila siku wilayani humo kwa madai ya kuingia hospitali ya wilaya bila kibali chake.

Desemba 12 mwaka huu, mwandishi mwingine wa Kituo kimoja cha Televisheni mkoani Arusha, alikamatwa na kushikiliwa na polisi katika kituo cha polisi cha Usa River wilayani Arumeru kwa tuhuma za kuandika habari zinazodaiwa kuwa ni za uchochezi huku agizo hilo likitolewa na mkuu wa wilaya hiyo, Alexander Mnyeti.

Desemba Mosi mwaka huu, mkuu wa wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama alimbana mwandishi wa gazeti mola la kila siku akimtaka aombe radhi kutokana na habari aliyoiandika kuhusu kutofanyika usafi wa mazingira kila mwisho wa mwezi kwa madai kuwa habari hiyo inalenga kumgombanisha na Rais Magufuli.

Naye mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alipokuwa mkuu wa wilaya ya Kinondoni aliwaweka rumande maofisa ardhi wa wilaya hiyo kwa saa sita kutokana na kuchelewa kufika katika eneo la Sangwe kata ya Wazo walipokuwa wamekubaliana kukutana kwa ajili ya kutafuta suluhisho la migogoro ya ardhi katika eneo hilo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo