Bima ya afya kutolewa kwa wote 2020


Edith Msuya

Bernard Konga
MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umepeleka mapendekezo serikalini ya kutungwa sheria itakayotoa fursa kwa kila mwananchi kuwa na bima ya afya.

Akizungumza jana Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bernard Konga, alisema mapendekezo hayo yako serikalini na kinachosubiriwa ni kukamilishwa taratibu, ili muswada ufikishwe bungeni.

Alisema wamefikia hatua hiyo baada ya kuona wananchi wengi hawana bima ya afya, hali inayosababisha baadhi yao kupata matatizo wanapopata maradhi.

"Tunataka muswada huu ufike bungeni ili sheria ipitishwe na kuwezesha asilimia kubwa ya wananchi kupata bima ili kuwapunguzia changamoto za ugonjwa," alisema.

Alisema lengo la Serikali si kuwalazimisha wananchi, bali kuwasaidia wapate huduma wanapopata matatizo na kuondokana kutegemea mtu mmoja mwenye fedha.

Kwa mujibu wa Konga, ifikapo mwaka 2020 matarajio ni kuhakikisha asilimia 85 ya Watanzania wanakuwa na bima ya afya.

"Serikali ina mtazamo mpana katika suala la afya nchini na Mfuko umejizatiti kuleta mapinduzi makubwa kwenye sekta ya afya kupitia mifuko yake katika kipindi cha miaka mitano ijayo," alisema.

Konga alisema hadi Desemba mwaka jana wanufaika wa mifuko hiyo ya NHIF na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF), walikuwa asilimia 27 ya Watanzania wote.

Hata hivyo, Mkurugenzi huyo aliasa wananchi wanaomiliki bima kutompa mtu mwingine hata ndugu, kwani kumpa mwingine ni kosa la jinai.

"Si ruhusa kwa mwananchi mwenye bima, kumpa mwenzake ni kinyume cha sheria na pia ni jinai," alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo