‘Aliyemwaga mboga’ mbele ya JPM atiliwa shaka


Mariam Cyprian, Tanga

TAHARUKI iliyojitokeza juzi mbele ya Rais John Magufuli, kwa mkazi wa Tanga, Swabaha Shosi kudai kudhulumiwa mirathi ya mumewe, imeibua sintofahamu mpya baada ya waliojiita familia ya huyo mume, kujitokeza na kutangaza kutomtambua Swabaha.

Akizungumza jana Tanga na mwandishi wa JAMBO LEO, mwanafamilia aliyejitambulisha kuwa mtoto katika familia hiyo, Saburia Mohamed (37), alidai mara ya kwanza kumwona Swabaha, ilikuwa siku ya kumaliza msiba wa baba yake.

Juzi katika kilele cha Siku ya Sheria, Swabaha huku akilia mbele ya Rais Magufuli na uongozi wa juu wa Mahakama na Polisi, alidai kunyimwa haki ya mirathi ya mumewe na vyombo vya kutoa haki nchini.

Swabaha ambaye alifanikiwa kugonga vichwa vya habari juzi na jana, alitaja vyombo vilivyomnyima haki kuwa ni Polisi, Mahakama, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).

Lakini jana Saburia, aliyejitambulisha kwa mwandishi wa gazeti hili kama mwanafamilia, alidai kutomtambua na kueleza kuwa siku ya kwanza kumwona, ilikuwa ya kumaliza msiba wa baba yao.

Saburia alidai kuwa siku hiyo Swabaha alitambulishwa kama binamu yao kwa shangazi yao aliyeko Mombasa na alikuwa akitoka eda Dar es Salaam baada ya kufiwa na mumewe.  

"Yule mama sisi kwa mara ya kwanza tulitambulishwa siku ya kumaliza msiba wa baba yetu tukiwa kwenye kikao cha familia, alifika saa sita mchana, tukaambiwa kuwa ni mjomba wa marehemu baba na ametoka eda Dar es Salaam ya aliyekuwa mumewe naye alithibitisha hilo," alidai.

Hata hivyo, Saburia alidai kuwa wakili wa familia alipokuwa akisoma wosia wa marehemu, Swabaha alimnyang'anya wosia huo na kukimbia nao baada ya kuona jina lake halimo.

Mtoto huyo alidai kuwa mwaka 2012 ilifunguliwa kesi ambayo ilimalizika kwa kufutwa Desemba 15, mwaka juzi na mwaka huo huo familia ilipeleka maombi Mahakama ya Mwanzo, kumpendekeza Saburia awe msimamizi wa mirathi.

Alidai kabla ya kupewa usimamizi, Swabaha alijitokeza mahakamani na kupinga kwa madai kuwa anayependekezwa kusimamia mirathi hiyo si mtoto halali wa marehemu.

Saburia alidai kuwa mama huyo hakuwa sahihi kupeleka taarifa kwa Rais, kwani kesi yao bado inaendelea Mahakama Kuu, ambako inasikilizwa na Jaji Amour Said Khamis na bado hukumu haijatolewa.

Alidai kuwa yeye na familia yake hawana vitisho vyovyote kwa mama huyo na familia ilipatwa na butwaa aliposema anahitaji ulinzi kwa kuwa anatishwa.

Mtoto huyo alielezea masikitiko yake kuwa ameumia baada ya Swabaha kumtangaza mbele ya Rais kuwa anahusika na uuzaji wa dawa za kulevya, kitu ambacho si kweli na kwamba yuko tayari kufanyiwa uchunguzi wa jambo hilo.

"Mimi ni mfanyabiashara wa nguo na nina duka langu la nguo barabara ya 14, ameniumiza sana pamoja na familia yangu kwa kusema nauza dawa za kulevya. Naomba Serikali iliangalie hili, kwani niko tayari kufanyiwa uchunguzi wa tuhuma hizi," alidai.

Mbali na Saburia, mwandishi wa habari hii alizungumza na aliyetambulishwa kuwa mke mkubwa katika familia hiyo, Mariam Juma ambaye alidai kuwa hamfahamu Swabaha.

"Mimi ninamfahamu mama yake ambaye ni wifi yangu na anaishi Mombasa, yeye sijawahi kumwona. Sasa nilishangaa kubadilika na kusema kuwa ni mke wa marehemu na kudai ananyanyasika kwa kudhulumiwa mirathi," alisema Mariam.

Aliitaka Serikali iingilie kati suala hilo ili wapate haki zao yeye na familia yake, ambayo ina watoto tisa na wake wawili.

Juzi Rais Magufuli aliwaagiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mkurugenzi wa Mashitaka, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini na Mahakama kupitia Jaji Kiongozi, kushughulikia jambo hilo ikiwa ni pamoja na kuhamishia kesi hiyo Mahakama ya Juu ili uamuzi ufanyike.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo