Mbunge: Tanroads wanahujumu uchumi Pwani


Sharifa Marira, Rufiji

MBUNGE wa Rufiji, Mohammed Mchengerwa ameeleza kusikitishwa kwake na kitendo cha  Wakala wa Barabara Nchini (Tanroads) mkoa  wa Pwani,  kutoa  kibali kwa taasisi ya walemavu ili kuvunja daraja lililojengwa kuelekea lilikopita bomba la gesi wilayani humo na kukiita ni uhujumu uchumi.

Daraja hilo lililojengwa kwenye kijiji cha Umwe Kusini kwa msaada wa Serikali ya China kwa zaidi ya Sh bilioni moja, lilivunjwa Novemba 28 mwaka jana na kusababisha wananchi kushindwa kuvuka kwenda eneo la bomba la gesi.

Akiwa katika eneo hilo, Mchengerwa alikabidhiwa barua ya Tanroads Mkoa kama kibali cha kuchukua chuma chakavu na makalvati mabovu.

Akisoma barua hiyo mbele ya wananchi wa eneo hilo, Mchengerwa  alisema barua hiyo iliyosainiwa na aliyekuwa  Meneja wa Tanroads wa Mkoa, Tumaini Sarakikya ilichangia  kubomolewa kwa daraja hilo baada ya Meneja huyo kuagiza kutafutwa kwa vyuma chakavu katika barabara za wakala huo.

"Barua hiyo ya Agosti 3 mwaka jana, ilielekeza kutafutwa vyuma chakavu katika barabara zilizo chini ya Wakala huo lakini si za Halmashauri kama ilivyofanyika kwenye eneo hilo," alisema Mchengerwa.

Alisema aina hiyo ya uharibifu wa miundombinu haukubaliki na kufananisha tukio hilo na uhujumu uchumi ambao hauvumiliki.

"Hii ni kesi ya uhujumu uchumi, kwa sababu ni uharibifu wa miundombinu, thamani ya uharibifu wa mali hii inafaa watu hawa kupelekwa katika Mahakama ya Mafisadi… wamekuja kuvunja daraja ambalo tulipata msaada wa zaidi ya Sh bilioni moja, kwa nini tunarudishwa nyuma?  Kwa sasa watu wanaokwenda lilipo bomba la gesi hawawezi kwenda, njia hakuna," alisema Mchengerwa.

Hata hivyo, Mbunge huyo alieleza kuwa alizungumza na Kaimu Meneja wa Tanroads wa Mkoa, Yudas Msangi ambaye alieleza kutofahamu jambo hilo na kutihusika na kibali hicho.

Msangi aliahidi kufuatilia jambo hilo akieleza kuwa huenda kuna watendaji wa ofisi yake wasio waaminifu wanaoshirikiana na watu wengine kufanya hujuma hizo.

Hata hivyo, pamoja na Msangi kukataa kujua jambo hilo, juzi maofisa waliojitambulisha kutoka Tanroads walifika eneo hilo wakiomba ushirikiano wa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM wa Wilaya ya Rufiji, Mussa Mng'eresa, kuangalia namna uharibifu ulivyotokea.

Akizungumzia suala hilo, Mng'eresa alisema: "Hawa watu waliojitambulisha wanatoka Tanroads ni bandia, lakini nashangaa wanatumia gari la Wakala huo wakati Kaimu Meneja anadai hana taarifa, hatuelewi hawa watu wanatuchanganya."
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo