CUF ya Lipumba yapewa ruzuku

Celina Mathew

MGOGORO ndani ya CUF umeendelea kuibua mapya baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi, Julius Mtatiro kueleza jinsi Profesa Ibrahim Lipumba alivyochukua fedha za ruzuku zaidi ya Sh milioni 300 Hazina bila utaratibu.

Amesema Bodi ya Wadhamini ya Chama hicho inakutana na kamati tendaji kutafakari ‘shambulio’ hilo kubwa la chama na kutekeleza hatua za kiutawala na kisheria za kuchukua na kwamba wanasheria wako tayari kupokea maelekezo kwa ajili ya kulinda chama.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Mtatiro alisema suala hilo ni la kushangaza kwa kuwa Oktoba 10 mwaka jana, Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi aliandika barua ya kusitisha utoaji ruzuku kwa chama hicho, akihofia migogoro iliyokuwa ikiendelea na kueleza kuwa hadi hali itakapokuwa shwari kiutendaji kuwezesha viongozi husika kusimamia matumizi ya fedha hizo ipasavyo ndipo ruzuku hiyo itatoka.

Aidha, alisema tangu Msajili aandike barua hiyo ya kusitisha ruzuku, chama kinaidai Hazina Sh milioni 635, kwa kuwa barua za usitishaji zipo na kwa kuwa CUF haitambui utaratibu mwingine wa kugawa ruzuku.

Alisema chama hicho kimeibiwa fedha za ruzuku Sh milioni 369 na zilitoroshwa kutoka Hazina ya Serikali Kuu Januari 5 na kuingizwa kwenye akaunti ya NMB tawi la Temeke yenye jina la The Civic United Front ikiwa na akaunti namba 2072300456.

"Bodi ya Wadhamini wa CUF ambayo ndiye msimamizi wa jumla wa masuala ya akaunti za fedha na mali za chama, haitambui akaunti hiyo na haikuwahi kuiidhinisha ipokee ruzuku ya CUF kutoka Serikali Kuu, Katibu Mkuu Maalim Seif Sharif Hamad ambaye ndiye mwajibikaji mkuu wa masuala ya kifedha na mali za chama, haitambui akaunti hiyo," alisema.

Aliongeza kuwa Maalim hajawahi kumwandikia Msajili au kumpa akaunti hiyo, aweke fedha za ruzuku ya CUF na kwamba vikao vya kitaifa vya chama kwa maana ya Kamati Tendaji ya Taifa na Baraza Kuu la Uongozi hawakuwahi kupitisha uamuzi huo wa fedha kuwekwa kwenye akaunti hiyo ya wilaya iliyoko NMB tawi la Temeke.

"Baada ya kugundua utoroshwaji huo wa fedha za ruzuku ya CUF ambazo ni za umma zenye masharti na taratibu zake katika kutolewa, tumejiridhisha kuwa akaunti ambayo Hazina walishiriki kuitumia kutorosha fedha za umma na mali za CUF, ni akaunti ya chama ambayo hutumiwa na wilaya ya Temeke kupokea mgao wa ruzuku kutoka chama Taifa," alisema.

Alisema CUF ina akaunti kila wilaya ya kichama, huku akitolea mfano Kinondoni yenye benki ambayo huitumia kupokea fedha zilizoidhinishwa na Kamati ya Utendaji ya Taifa ya Chama kwa mujibu wa Katiba, wilaya ya Ilala pia ina akaunti ya aina hiyo, Mtwara na mikoa mingine.

Alisema baada ya watu wanaomsaidia Profesa Lipumba ambaye alimwita 'Bwana yule' kuona kwamba Bodi ya Chama imezuia njama za ufunguaji akaunti mpya ya CUF, walitumia mbinu mpya ya aina hiyo hiyo kwa njia tofauti na siku mbili kabla ya utoroshwaji wa fedha hizo, waliondoa baadhi ya viongozi Temeke kwenye kusaini akaunti hiyo.

Alieleza kuwa uondoaji viongozi hao ulikwenda sambamba na kugeuza baadhi ya wateule wa Lipumba wanaofanya kazi za kuhujumu chama kutokea Buguruni, kuwa watia saini wa akaunti ya wilaya ambao ni Mbunge wa Kaliua, Magdalena Sakaya na Thomas Malima.

Alisema siku moja baada ya NMB na wala njama kukamilisha mchakato wa kubadilisha watia saini wa akaunti ya CUF inayomilikiwa na wilaya ya Temeke, Hazina iliweka fedha hizo bila kuchelewa na siku hiyo hiyo watia saini wapya wa akaunti ya NMB Temeke, waliulizia kiasi cha fedha kilichomo kwenye akaunt hiyo na walifanya hivyo kwenye tawi la Barabara ya Mandela.

Alifafanua kuwa siku iliyofuata Januari 6 watia saini hao wakiongozwa na Malima walikwenda NMB Temeke na kutoa Sh milioni 69 kisha wakahamisha Sh milioni 300 kutoka akaynti namba 41401600207 kwenda kwenye akaunti ya mtu binafsi aliyejulikana kwa jina la Mhina Omary ambaye ni Diwani wa CUF wa Wilaya ya Handeni.

Zahamishwa

Akizungumzia namna Omary alivyohamisha fedha alifafanua kuwa Januari 6 aliondoa Sh milioni 100 kutoka NMB tawi la Magomeni, akaongeza Sh milioni 50 kisha akaelekea tawi la Kariakoo na kutoa Sh milioni 100 na kuongeza akaongeza milioni 49.5.

Alisema wakati Omary anazunguka kwenye matawi hayo kutoa fedha alikuwa na ulinzi wa polisi waliovalia kiraia kwenye magari ya CUF akifuatana na Malima chini ya usimamizi wa watu wawili ambao ni Sakaya na Kambaya.

Alisema baada ya fedha hizo kuhamishwa akaunti yake ilibaki na Sh 207 kama zawadi kwa kuwa wakati anaweka Sh milioni 300 hakukuwa na hata senti tano na kwamba fedha zilizotoroshwa na kupelekwa kusikojulikana ilikuwa ni kabla chama kupata taarifa kuhusu wizi huo.

JAMBO LEO ilimtafuta Profesa Lipumba ili kutolea ufafanuzi suala hilo, simu yake iliita bila majibu lakini Kambaya alisema ni kweli fedha hizo waliomba Hazina kwa kuwa Lipumba anatambulika kama Mwenyekiti wa Chama.

"Nashangaa sana mnashindwa kuelewa nini, fedha tumeomba na tumepewa kwa ajili ya shughuli za kichama si vinginevyo, kwa kuwa Lipumba ni Mwenyekiti wa Chama," alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo