Ally Daud wa MAELEZO
Ummy Mwalimu |
MIKOA na halmashauri nchini zimetakiwa
kuweka hadhari ya kipindupindu kwa kuzingatia usafi binafsi na wa mazingira
hasa wakati wa mvua za vuli na msimu wa sikukuu za mwisho wa mwaka ili kuepuka ugonjwa
huo.
Hayo yamesemwa jana Dar es Salaam, na
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, kwenye
mkutano na waandishi wa habari kuhusu mwenendo wa kipindupindu kwa Novemba.
Waziri Ummy alisema mikakati ya
kudhibiti ugonjwa huo ishirikishe sekta za afya bila kusahau jamii na
kuhakikisha kila halmashauri inaunda na kuimarisha Kamati ya Afya ya Kata.
Aliiagiza mikoa na halmashauri zote
nchini kutoa taarifa ya wagonjwa wapya wa kipindupindu ili jitihada za makusudi
za kupambana na ugonjwa huo zifanyike mapema ili kujenga Taifa lisilo na
magonjwa ya mlipuko.
Alisema takwimu zinaonesha kuwa Novemba
mikoa sita ilikuwa na wagonjwa ambayo ni Morogoro 282, Dodoma 96 na vifo 2,
Mara 31, Kigoma 30 na vifo 4, Arusha 11 na Dar es Salaam 8 kutoka wagonjwa 250 na vifo 4 kwa Oktoba.
Wakati
huo huo, Waziri Ummy alipokea vifaa vya matibabu ya
mabadiliko ya awali ya saratani ya mlango wa kizazi vyenye thamani ya takribani
Sh milioni 100 za kitanzania kutoka shirika la kimataifa la Pink Ribbon Red
Ribbon ili kupambana na ugonjwa huo nchini.
Akikabidhi msaada huo, Mtendaji Mkuu wa
Shirika hilo, Celina Schocken alisema walitoa vifaa hivyo ili kuisaidia nchi
juhudi zake za kupambana na saratani ili kuokoa maisha ya wanawake.
0 comments:
Post a Comment