Sheria mpya isiwatishe wanahabari


Salha Mohamed

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF)
WANAHABARI wameaswa kutoogopa na kukatishwa tamaa na vifungu vichache vya Sheria ya Habari iliyosainiwa na Rais John Magufuli hivi karibuni, badala yake wanatakiwa kuisoma sheria hiyo na kuielewa.

Hayo yalibainishwa Dar es Salaam jana na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (TEF), Theophil Makunga, wakati wa mkutano wa siku mbili uliowakutanisha wahariri wa vyombo vya habari hapa nchini.

Mkutano huo wa wahariri ulioanza jana na kumalizika leo, umelenga kupitia sheria ya huduma za vyombo vya habari na kujadili mpango mkakati wa TEF, wa kuendeleza tasnia ya habari, huku wakipata uzoefu kutoka nchi za Kenya na Afrika Kusini.

Kupitia mkutano huo, Makunga alisema hakuna haja ya wanahabari kuogopa au kuwa na wasiwasi kuhusu sheria hiyo iliyosainiwa hivi karibuni na Rais John Magufuli.

“Kama tuliweza kuishi na sheria ya magazeti ya mwaka 1976 basi tunaweza hata chini ya hii sheria mpya….kwa sababu hii sheria ni afadhali kuliko ile ya mwaka 1976.

“Imepunguza vitu vingi sana ambavyo vilikuwa amepewa mtu mmoja na badala yake kuhamishiwa kwa bodi, hivyo kuna vitu ambavyo ni vizuri katika hii sheria kuliko ile ya mwaka 1976,”alisema.

Makunga alifafanua kuwa awali katika muswada wa habari, suala la elimu lilionesha kuwa ni lazima  mwandishi afike ngazi ya Stashahada huku sheria ikiwa haijaonesha hivyo.

Makunga aliongeza kuwa wanasubiri kanuni za sheria hizo zitasemaje huku akibainisha kuwa angependa kipengele cha elimu kiwe na ngazi ya mwandishi gani anafanya nini kwa wakati gani.

“Hakuhitaji stashahada kwenda kuandika habari pale kambi ya fisi. Ila kwa mhariri suala la stashahada ni jambo zuri, kwani itamsaidia kuwa na upeo mkubwa wa kutoa uamuzi, mwandishi si lazima,”alisema.

Makunga alisema katika sheria hiyo kuna vipengele vichache hatarishi kwa mwandishi, huku akibainisha kuwa vinaweza kufanyiwa marekebisho ya vifungu kama serikali itakubali.

Aliongeza kuwa tayari sheria ya habari imesainiwa kinachotakiwa ni kuona namna ya kuendesha tasnia ya habari na kuimarika chini ya sheria hiyo bila kuathiri uendelezaji wa taaluma ya waandishi wa habari.

Mwanahabari mpekuzi wa nchini Kenya, Mohamed Ali alisema waandishi wa habari wa Tanzania ni waoga zaidi duniani.

“Tanzania ipo ambapo Kenya ilikuwa miaka ya 1980, ambapo hakukuwa na uhuru wa habari na thulma ya kila aina ikiwemo kuuwa,”alisema.

Alisesma nchini kwao walipinga na kutaka kuwa na uhuru wa kuzungumza na walifaulu ingawa kulikuwa na changamoto ndogo ndogo.

“Ukiangalia Tanzania wamekubali kuwa waoga kila mtu atasema hakuna shida, lakini hakuna mtu anayeweza kusimama na kusema anaweza kukomboa kwa niaba ya taifa zima,”alisema.

Aliongeza kuwa Watanzania wanahitaji kukataa sheria hizo ambazo zitagandamiza haki ya kila Mtanzania kama ambavyo wao walikataa na kuzikataa sheria hizo.

“Ni jukumu lenu Watanzania msimame hizi sheria si za wanahabari bali ni za Tanzania, maana ukimzima mwanahabari umezima Tanzania,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo