Profesa Lipumba azua kizazaa Ukawa



Fidelis Butahe na Suleiman Msuya


Profesa Ibrahim Lipumba
WAKATI Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ikitangaza ratiba ya uchukuaji fomu kujaza nafasi ya mbunge na madiwani zilizo wazi, vyama vinavyounda Ukawa viko mtegoni kutokana na mgogoro uliokigawa Chama cha Wananchi (CUF).

Jana baadhi ya viongozi wa vyama vinavyounda Ukawa vya Chadema, NLD na NCCR-Mageuzi viliiambia JAMBO LEO kuwa vitashirikiana katika uchaguzi huo mdogo na Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, na si Mwenyekiti wa Chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba.

Wakati viongozi hao wakieleza hayo, Naibu Katibu Mkuu wa CUF -Bara, Magdalena Sakaya  anayemuunga mkono Profesa Lipumba, alisema chama hicho kitafanya vikao kwa mujibu wa Katiba ili  kupata wagombea kwenye uchaguzi huo, kauli ambayo ilipingwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya Chama hicho, Julius Mtatiro.

Katika uchaguzi mkuu mwaka jana, vyama hivyo vilishirikiana kusimamisha mgombea mmoja kwenye baadhi ya majimbo na kata huku kwa pamoja vikimpitisha na kumuunga mkono mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa.

Mgogoro ndani ya CUF ulianza baada ya Profesa Lipumba kuandika barua ya kutaka kurejea kwenye uenyekiti, ikiwa imepita miezi 10 baada ya kujiuzulu, jambo ambalo lilizua mgogoro mkubwa, ikiwa ni pamoja na kuvunjika kwa Mkutano Mkuu uliompitisha Mtatiro kuwa Mwenyekiti.

Baada ya mvutano huo, Baraza Kuu la Uongozi la Chama hicho lilimvua uanachama Profesa Lipumba na baadaye kumfukuza uanachama, huku Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ikitoa tamko la kumtambua kuwa mwenyekiti wa CUF.

Kwa tamko hilo la Msajili, Baraza la Wadhamini la CUF lilifungua kesi Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kupinga kurejeshwa kwa Lipumba.

Kutokana na mvutano huo, jana baadhi ya viongozi wa Ukawa walitoa msimamo kuhusu uchaguzi huo katika jimbo la Dimani, Zanzibar na kwenye kata 22.

Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Danda Juju alisema: “Chama chetu hatuamini uwepo wa Lipumba katika CUF. Kama chama, tutaendelea na ushirikiano wa Ukawa ikiwa ni pamoja na kuamua mgombea wa chama gani agombee kulingana na taratibu tulizojiwekea.”

Juju alisema Mtendaji Mkuu wa CUF ni Katibu Mkuu si Mwenyekiti na katika vikao vyote vya Ukawa, wamekuwa wakishirikiana na Maalim Seif, hivyo hakuna uwezekano wa kuungana na Lipumba.

Kauli hiyo iliungwa mkono na Katibu Mkuu wa NLD, Tozi Mtwange na kusisitiza kuwa Profesa Lipumba aliondolewa na vikao vya CUF kwa mujibu wa Katiba, hivyo hawawezi kushirikiana naye katika uchaguzi huo.

Mtatiro alisema: “Chama kitakutana kupitisha wagombea. Hao wengine (wafuasi wa Profesa Lipumba) hawawezi kufanya vikao vya uamuzi.”

Alisema vikao hivyo vitaanza muda wowote kuanzia sasa na kusisitiza kuwa ushirikiano wa Ukawa kwenye kata na jimbo hilo utaendelea kama ilivyokuwa kwenye Uchaguzi Mkuu, ikiwa ni baada ya viongozi wake kukutana na kupanga wagombea wa chama gani watakaopeperusha bendera za vyama vyao na Ukawa katika uchaguzi huo.

Kauli ya Mtatiro ilipingana na ya Sakaya ambaye awali alilieleza gazeti hili kuwa vikao vya kupitisha wagombea wa CUF kwenye kata hizo vitafanyika kwenye wilaya husika, kwamba kwa mgombea wa   Dimani, uamuzi utatolewa na uongozi wa chama hicho kwenye jimbo hilo.

Kwa mujibu wa ratiba ya NEC, fomu za uteuzi kwa ajili ya uchaguzi huo zitaanza kutolewa Desemba 10 hadi 22 ukifuatiwa na uteuzi wa wagombea Desemba 22, wakati Desemba 23 hadi Januari 21 ni muda wa kampeni ambapo Januari 22, itakuwa siku ya kupiga kura.

NEC itaendesha uchaguzi mdogo kujaza nafasi za wazi za udiwani kwenye kata 22 katika baadhi ya halmashauri za Tanzania Bara zilizokuwa wazi kutokana na sababu mbalimbali.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo