Magufuli atishia kumtumbua Waziri


* Ni Kama hatasitisha timuatimua ya wamachinga
* Ambana Muhongo kuhusu mwekezaji wa madini

Waandishi Wetu

RAIS John Magufuli ametishia ‘kuwatumbua’ Waziri na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi).

Amesema ‘atawatumbua’ ikiwa watashindwa kusitisha mchakato wa kuondoa wamachinga katika maeneo mbalimbali nchini, huku akimweka kikaangoni Waziri wa Nishati na Madini kuhusu mwekezaji.

Kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu, Rais Magufuli alionya kuwa kiongozi asiye tayari kutekeleza maagizo yake, aachie ngazi.

Hata hivyo, Rais Magufuli alisema maagizo yake hayana maana kuwa wamachinga na wachimbaji wadogo wanaruhusiwa kuendesha shughuli zao kwa kuvunja sharia, bali wazingatie sheria na mamlaka zisinyanyase wanyonge.

Agizo hilo limekuja siku chache baada ya wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa manispaa za Nyamagana na Ilemela, Mwanza kuvunja vibanda vya wafanyabiashara hao usiku wa manane na kudaiwa kuharibu mali zao.

Uvunjaji huo wa usiku wa maeneo ulilalamikiwa na wafanyabiashara hao huku wakidai kuwa maeneo wanayopelekwa hayafai kwa biashara na kuwa hakuna maandalizi yaliyofanyika kwa ajili ya biashara zao.

Rais Magufuli alitoa agizo hilo jana akiwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan na kubainisha kuibuka tabia ya baadhi ya wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi, kufukuza wamachinga bila utaratibu.

Alisema mchakato wa kuhamisha wamachinga unatakiwa kufanyika pale ambapo mamlaka husika zimekamilisha maandalizi ya maeneo wanayohamishiwa kwa kushirikisha wamachinga wenyewe.

“Wakati mwingine mnawapeleka maeneo ya mbali ambayo hayafai hata kwa biashara, hili jambo si sawa hata kidogo.

"Sipendi wamachinga wafanye biashara kwenye hifadhi za barabara, lakini hakuna sheria katika nchi hii, inayosema mtu wa biashara ndogo ndogo au mmachinga hatakiwi kukaa katikati ya mji, tukianza kwenda kwenye utaratibu wa namna hiyo, maana yake tunaanza kutengeneza madaraja ya Watanzania,” alisema.

Alisema utaratibu huo utaanza kuonesha kuwa kuna Watanzania fulani wa daraja fulani wanapaswa kukaa katikati ya mji na Watanzania wa daraja fulani hawatakiwi kukaa katikati ya mji.

“Huo si mwelekeo wetu na wala Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo mimi na wewe (Makamu wa Rais) tulipita kuinadi, haisemi tutengeneze madaraja ya watu wanaostahili kukaa mjini na wengine hawastahili kukaa mjini, sasa nimeona hili nilizungumze na nataka kulirudia kwa mara ya mwisho," alionya Rais Magufuli.

Dk Magufuli alielekeza kuwa wamachinga waliondolewa kwenye maeneo yao Mwanza waachwe waendelee na shughuli zao mpaka hapo Halmashauri ya Jiji la Mwanza, itakapokamilisha maandalizi ya mahali watakapohamishiwa na kwa kuwashirikisha wamachinga wenyewe.

"Narudia, na hii ni mara ya mwisho, kawaambieni hata wamachinga wa Mwanza warudi kwenye maeneo yao, mpaka watakapowatengenezea utaratibu mzuri,” alisema.

Rais alisema Kigamboni palikuwa na wamachinga na walihama vizuri na kutengenezewa miundombinu yao katika soko lao na sasa hivi wanafanya kazi vizuri.

Alisema mafanikio ya Kigamboni yamechangiwa na ushirikishwaji wa viongozi wa wamachinga, lakini Mwanza imekuwa ni amri tu na wengine wanatumia hata usemi wa ‘Hapa Kazi Tu’.

“Mimi sikusema usemi wa ‘Hapa Kazi Tu’ wa namna hiyo, nadhani mmenielewa," alisisitiza Rais Magufuli alipokuwa akiwaekeleza Naibu Waziri wa Tamisemi, Suleiman Jaffo na Katibu Mkuu, Mussa Iyombe.

Katika hatua nyingine, Rais Magufuli aliagiza Wizara ya Nishati na Madini kusitisha mara moja mchakato wa kuondoa wachimbaji wadogo kwenye kijiji cha Nyaligongo kata ya Mwakitolyo mkoani Shinyanga.

Alitaka wachimbaji hao waachwe waendelee na shughuli zao na kuagiza leseni ya mwekezaji ifutwe na anayedai eneo hilo ni lake aondolewe.

“Wale waliofukuzwa Shinyanga wabaki palepale, kama ni leseni ya huyo mwekezaji ifutwe, Makamu wa Rais fuatilia hili, mweleze Waziri husika (Profesa Sospeter Muhiongo), waache kufukuza wananchi hovyo hovyo, wale wanapata riziki yao, wanasomesha watoto wao lakini wanafukuzwa tu.

“Na hizi ndizo ajira zenyewe, tulisema tunatengeneza ajira, wewe mwekezaji ni mmoja, unakwenda kufukuza watu 5,000! Haiwezekani na wala haingii akilini,” alisisitiza Rais Magufuli.

Rais pia alikemea vitendo vya wawekezaji wakubwa kupewa maeneo ambayo wachimbaji wadogo wanaendesha shughuli zao, wakifanya hivyo kwa mtindo wa kutengeneza nyaraka zinazoonesha mwekezaji husika alipewa eneo hilo kabla ya wachimbaji wadogo na kusisitiza kuwa mchezo huo hautavumiliwa.

Simbachawene

Wakati huo huo, Waziri wa Tamisemi, George Simbachawene alikiri kukutana na Rais Magufuli ambako alielezwa kuwa hafurahishwi na jinsi wakuu wa mikoa, wilaya na wenyeviti wa serikali za mitaa wanavyonyanyasa wamachinga.

Simbachawene alisema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam akisema Rais anataka viongozi na watendaji kuangalia utaratibu mzuri wa kushirikisha wajasiriamali hao ili kupata ufumbuzi shirikishi zaidi.
“Kwa kuanzia ni vema yakatengwa maeneo ya katikati ya mji yenye wateja wa bidhaa zinazouzwa, kwa kuangalia uwezekano wa kufunga mtaa japo mmoja ili utumike kwa kazi za kimachinga,” alisema Simbachawene.

Alisema usumbufu unaojitokeza maeneo mbalimbali unasababisha wananchi kupoteza mitaji yao ambayo wengine wamekopa kwenye vikundi vya vicoba na hivyo kuhatarisha mustakabali wa maisha yao na familia zao.

Aliongeza kuwa mamlaka zinatakiwa ziandae maeneo rafiki yenye mahitaji muhimu, ili yaweze kufikika kirahisi na kuruhusu biashara kufanyika bila shida kabla ya kuhamasisha wafanyabiashara kwa njia shirikishi zaidi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo