CCM kuja na Sekretarieti yenye sura mpya


Mwandishi Wetu

VIKAO vya kwanza vya CCM tangu Rais John Magufuli achaguliwe kuwa Mwenyekiti, vitakavyoanza Jumapili Dar es Salaam, vinatarajiwa kufanya mabadiliko ya Sekretarieti yake, huku sura kadhaa zikitajwa kuwemo, JAMBO LEO limedokezwa.

Rais Magufuli ambaye alichaguliwa Julai 23 kuwa Mwenyekiti wa CCM, aliitaka Sekretarieti ya Chama hicho yenye wajumbe wanane chini na Katibu Mkuu, Abbulrahman Kinana isiondoke, lakini uamuzi wa kuitisha kikao hicho unaelezwa huenda ukaja na mabadiliko makubwa.

Mabadiliko hayo yanachagizwa zaidi na uteuzi wa Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho, Rajab Luhwavi kuwa balozi sambamba na Dk Emmanuel Nchimbi, Dk Pindi Chana na Dk Asha-Rose Migiro ambao walikuwa wajumbe wa Kamati Kuu. Lakini pia Katibu wa Itikadi an Uenezi, Nape Nnauye ambaye ni Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili, zilieleza kuwa uteuzi huo ni ishara kwa chama hicho kuanza mchakato wa kusaka makada wengine wa kuziba nafasi hizo, kama ilivyopata kutokea miaka ya nyuma, hasa wajumbe wa Sekretarieti walipoteuliwa kuwa mawaziri.

Zilieleza kuwa miongoni mwa watu wanaoweza kuingia katika Sekretarieti mpya ni pamoja na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi anayetajwa kwa nafasi ya Katibu Mkuu na Mkuu wa Mkoa wa Wilaya ya Ubungo Humphrey Polepole, anayetajwa huenda akarithi mikoba ya Nape.

Wengine ni Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Makala na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi, Abdallah Bulembo.

“Unakumbuka Dk Migiro alipovaa viatu vya January Makamba (Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira na Muungano) kwenye nafasi ya Katibu wa Siasa na Mambo ya Nje.

“Wakati ule Makamba aliachia nafasi ili abaki na ya Unaibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia,” kilieleza chanzo chetu.

Kilifafanua kuwa Dk Migiro baada ya kuteuliwa kuwa balozi Uingereza, nafasi yake ilikaimiwa na Dk Chana ambaye ameteuliwa kuwa balozi pia.

“Kwa sasa Nape (Nnauye) ni Katibu wa Itikadi na Uenezi na pia ni Waziri wa Habari, hivyo inawezekana nafasi yake ndani ya chama akachukua mtu mwingine. Si ajabu Polepole hata Ole Sendeka (Christopher) ambaye kwa sasa ni msemaji wa CCM,” alisema mtoa habari huyo.

Taarifa hizo pia zilitolea mfano wa jinsi Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba alivyoachia mikoba ya Katibu wa NEC wa Uchumi na Fedha kwa Zakia Meghji, baada ya kuwa waziri.

Katika mabadiliko hayo, taarifa hizo zinamtaja Lukuvi kuchukua nafasi ya Kinana kutokana na utendaji wake na kuijua CCM vilivyo licha ya kuwa Katibu Mkuu huyo alichangia kwa kiasi kikubwa kurejesha nguvu za chama kipindi cha miaka mitano alichoshika nafasi hiyo.

Kinana amekuwa Katibu Mkuu tangu mwaka 2012, akiongoza kampeni ya kuwaaminisha wananchi kuwa CCM ina sera nzuri, huku akishutumu hadharani viongozi wa Serikali kuwa wanakwamisha maendeleo ya nchi.

Wengi wanaamini kuwa kampeni hiyo ilichangia kuifanya CCM ikabiliane na ongezeko la nguvu ya Upinzani hata kushinda uchaguzi mkuu uliopita.

Baada ya Rais Magufuli kukabidhiwa uenyekiti wa CCM, aliikubali kazi iliyofanywa na Sekretarieti hiyo na kuitaka iendelee, iwapo ataamua kumpumzisha kwa sasa huenda makada hao wakaula kwa kuzingatia ukada na uzoefu wao.

Lukuvi ni miongoni mwa wanaopewa nafasi kubwa kutokana na uzoefu wake ndani ya chama, akiwa ameanzia Umoja wa Vijana, ukuu wa mkoa hadi uwaziri.

Taarifa hizo zinabainisha kuwa Makala ana nafasi kubwa ndani ya chama hicho kwa kuwa alianzia UVCCM hadi kuwa mweka hazina wa CCM na baadaye naibu waziri.

Makala alishindwa kwenye uteuzi wa ubunge wa Mvomero ndani ya CCM na baadaye kuteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kabla ya kuhamishiwa Mbeya.

“Bulembo naye si mtu wa kubeza kwa sababu anaelewana vema na Rais na pia ana uzoefu ndani ya chama. Kama utakumbuka alikuwa karibu na Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita,” zilieleza taarifa hizo.

Wajumbe wa Sekretarieti hiyo iliyo chini ya Kinana ni Vuai Ali Vuai, ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Luhwavi, Mohamed Seif Khatib (Katibu wa Oganaizesheni wa Halmashauri Kuu), Migiro, Meghji na Nape.


Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo